Gachagua atoa makataa kwa wanaohamia DCP
KIONGOZI wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, ameongeza kwa siku 10 mkutano wake wa kisiasa unaoendelea katika makazi yake ya Wamunyoro, Kaunti ya Nyeri, huku akitoa onyo kwa viongozi wanaotaka kuhamia chama hicho kwamba muda wa kufanya uamuzi unakaribia kuisha.
Bw Gachagua alisema aliongeza muda huo kufidia siku alizotumia kusherehekea ushindi wa DCP katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou ambao mgombea wa chama hicho, Kamau Ngotho, alishinda mgombea wa UDA. Pia alisema alitumia muda kuzuru kaunti za Embu, Meru na Tharaka Nithi kupinga juhudi za kutenganisha kisiasa eneo la Mlima Kenya Mashariki.
Akizungumza katika mahojiano ya moja kwa moja na mchambuzi wa siasa Herman Manyora, Bw Gachagua alisema masuala mawili makuu yanayojadiliwa katika mkutano huo ni nani anayefaa kuungwa mkono kuwania urais mwaka wa 2027 na masharti ambayo Mlima Kenya utaweka iwapo haitatoa mgombea wa urais.
“Kuna upungufu mkubwa wa imani katika siasa. Wananchi wengi wanasema wanatamani niwaongoze, lakini pia ninaelewa kuwa Mlima Kenya hauwezi kushinda urais peke yake. Tutahitaji kushirikiana na maeneo mengine,” alisema.
Alisisitiza kuwa yuko tayari kuacha azma yake ya kuwania urais ikiwa hatua hiyo itasaidia kuondoa serikali ya Rais William Ruto kupitia uchaguzi.
“Hata hivyo, kura za Mlima Kenya hazitatolewa bure. Tutataka kujua wananchi wetu watanufaika vipi kutokana na ushirikiano huo,” alisema.
Kwa mujibu wake, mazungumzo hayo hayatakuwa kuhusu ugavi wa nyadhifa za kisiasa pekee bali pia masuala ya uchumi yanayowagusa wananchi wa eneo hilo.
“Tutazungumzia kodi, mazingira bora ya biashara, usalama wa wafanyabiashara, bei ya uhakika ya mazao na mikopo nafuu. Hayo ndiyo mambo tunayopigania,” alisema.
Bw Gachagua pia alitangaza kuwa ameongeza hadi katikati ya Agosti muda aliowapa viongozi wanaotaka kuhamia DCP. Alisema anahitaji kujua idadi ya wagombeaji watakaotumia tiketi ya chama hicho ili kupanga bajeti ya kampeni, ambayo anakadiria kufikia Sh4 bilioni.
Aidha, alidai kuwa baadhi ya Mawaziri na Makatibu wamekuwa wakimtafuta kwa siri wakitaka kujiunga na DCP, lakini akawataka watangaze hadharani uamuzi huo.
“Wengine wanakuja usiku. Nimewaambia kama kweli wanataka kuhamia DCP wafike mchana mbele ya kamera ili bosi wao aone wakihama,” alisema.
Kauli hizo zimezua mjadala ndani ya chama hicho. Seneta wa Murang’a, Joe Nyutu alipinga viongozi waliokuwa waaminifu kwa serikali kupewa nafasi katika DCP, akisema wanachama waliobaki na Bw Gachagua wakati wa kipindi kigumu hawapaswi kusukumwa pembeni.