Jamvi La Siasa

Je, Ruto anajaribu ‘kumpanga’ Mudavadi kumrithi 2032?

Na CECIL ODONGO August 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

JE, Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi ndiye mwanasiasa mwenye ushawishi mkubwa zaidi katika serikali ya Rais William Ruto kwa sasa?
Swali hilo limeibuka kufuatia madai kwamba baadhi ya majukumu muhimu ya uratibu wa shughuli za serikali yaliyokuwa yakisimamiwa na afisi ya Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki sasa yamehamishiwa na kuwekwa chini ya himaya ya Bw Mudavadi.
Hatua hiyo imezua mjadala mpya kuhusu iwapo mwanasiasa huyo ndiye anaaminiwa zaidi na Rais Ruto katika utawala wa Kenya Kwanza.
Bw Mudavadi amekuwa mwenyeji wa Rais Ruto katika ziara zake Magharibi mwa Kenya huku Profesa Kindiki akikosa ziara hizo.
Wikendi iliyopita alimkaribisha Rais Ruto katika Kaunti ya Busia wakati wa kutawazwa kwa Askofu wa Dayosisi ya Katakwa ya Kanisa la Anglikana, Vitalis Job Ekuru, na baadaye akamkaribisha kuhutubia waumini pamoja na mkutano wa hadhara mjini Amagoro.
Awali, Juni 13, Bw Mudavadi pia alikuwa mwenyeji wa Rais katika Chuo Kikuu cha Masinde Muliro wakati wa uzinduzi wa Chama cha Ushirika cha Shirikiana.
Katika hafla mbalimbali za umma, Rais Ruto amekuwa akimtaja Bw Mudavadi kwa jina lake la heshima la kitamaduni, “Omwami”, jambo ambalo linaonyesha ukuruba wa kisiasa kati ya wawili hao.
Ushawishi wa Bw Mudavadi uliongezeka zaidi Oktoba 5, 2024 baada ya Rais kumkabidhi Wizara ya Masuala ya Nje kutoka kwa Waziri Alfred Mutua.
Tangu wakati huo, amekuwa akiongoza shughuli za kidiplomasia za Kenya na ameandamana na Rais katika karibu kila ziara muhimu ya nje. Wakati mwingine amekuwa akisafiri mapema kuandaa mikutano mataifa ya nje kabla ya ujio wa rais.
Mbunge wa Emuhaya Omboko Milemba alipuuza madai kuwa kinara huyo wa mawaziri kuongezwa majukumu kunaashiria Rais anapanga kumpiga kumbo Profesa Kindiki.
“Hata Profesa Kindiki alisema haya ni mabadiliko ya kawaida ya kiutawala. Mudavadi ni mmoja wa nguzo kuu za serikali hii na kupewa majukumu zaidi hakufai kuzua maswali,” akasema Bw Milemba.
Mbunge huyo alisema uamuzi wa Bw Mudavadi kutowania wadhifa wowote wa 2027 unampa nafasi ya kujikita kikamilifu katika kuratibu shughuli za serikali na kusukuma mbele ajenda ya Rais Ruto.
Hatua imefufua kumbukumbu
Kuongezwa kwa majukumu ya Bw Mudavadi pia kumefufua kumbukumbu za utawala wa mwisho wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, ambapo aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i alipewa mamlaka ya kusimamia shughuli za serikali huku aliyekuwa Naibu Rais William Ruto akionekana kutengwa kuelekea uchaguzi wa 2022.
Mbunge wa Khwisero Christopher Aseka naye anasema Rais Ruto anamtegemea Bw Mudavadi katika kuratibu wa shughuli za serikali, utekelezaji wa sera na masuala ya kiutawala, huku akimtegemea Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya na Spika wa Bunge la Taifa Moses Wetang’ula kuimarisha ushawishi wake kisiasa Magharibi.
Hata hivyo, Bw Aseka amemwonya Bw Mudavadi asidhani kuwa nafasi yake ya sasa itamhakikishia moja kwa moja uungwaji mkono wa kisiasa 2032.
Kwa mujibu wa Bw Aseka, kuongezwa kwa idara chini ya usimamizi wa Bw Mudavadi ni ishara ya imani kubwa ambayo Rais Ruto anayo kwake.
Bw Mudavadi tayari ametangaza kuwa hatawania urais wala nafasi ya naibu rais 2027, akisema lengo lake ni kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2032.
“Mimi silengi wadhifa wa nambari mbili, nalenga kuwa namba moja kwa sababu nimewahi kuwa makamu wa rais. Mimi nalenga uongozi wa nchi mnamo 2032,” akasema Bw Mudavadi mwezi uliopita akiwa katika ziara kwenye Kaunti ya Trans Nzoia.
wa mujibu wa mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Lumala Masibo, Rais Ruto analenga kutumia Bw Mudavadi kutuliza joto kali kati ya mirengo ya ODM na UDA kuhusu nafasi ya naibu rais.
 “Ukiangalia vizuri kwa sasa Profesa Kindiki anafanya kila awezalo kuhakikisha kwamba anamdhihirishia rais eneo la Mlima Kenya Mashariki lipo nyuma yake. Kwa upande mwingine mrengo wa ODM nao unasaka nafasi hiyo,
 “Hii ina maana kuwa Bw Mudavadi ndiye anaweza kumakinikia mengi ya majukumu ya serikali kwa sababu naye hawanii wadhifa wowote wa kisiasa 2027,” akasema Profesa Masibo.