Wadau wapinga hatua ya serikali ya kutaka watalii wanaoingia nchini kuwa na bima ya lazima
WADAU katika sekta ya utalii wamepinga vikali uamuzi wa serikali wa kutaka wageni wote wanaoingia nchi kuwa na bima ya lazima wakionya kuwa hatua hiyo itaathiri nchi kuvutia watalii wa kimataifa.
Kulingana na tangazo lililochapishwa kwenye Gazeti Rasmi la Serikali la Julai 30, 2026 na kutiwa sahihi na Waziri wa Afya, Bw Aden Duale, wageni wote wanaoingia humu nchini watalazimika kuwa na bima ya afya yenye kiwango cha chini cha karibu Sh6.45 milioni.
Bima hiyo itagharamia hadi Sh2.58 milioni za matibabu, Sh3.22 milioni za usafiri wa dharura wa mgonjwa, Sh38,700 za dawa zilizoagizwa na daktari, Sh129,000 za matibabu ya afya ya akili na Sh645,000 za kusafirisha mwili wa marehemu kurejeshwa nchini kwao.
Kulingana na serikali, hatua hiyo inalenga kuhakikisha watalii wanapata huduma wanapokumbwa na dharura za kiafya.
Hata hivyo, wadau wa utalii wamejitokeza na kupinga hatua hiyo wakisema itaongeza gharama za kuzuru Kenya.
“Hatua hii itaongeza gharama kwa watalii. Kama sekta ya utalii tunapinga hatua hii. Huu si mwelekeo unaofaa, tunafaa kuweka mikakati ya kuvutia watalii si kuwazuia kuzuru nchi yetu,” Mkurugenzi Mtendaji wa chama cha wamiliki wa hoteli na wahudumu (KAHC), Dkt Sam Ikwaye, alisema.
Wadau hao walisema bima hiyo ya lazima inaongezwa juu ya ada nyingine ambazo wageni tayari hulipa, ikiwemo ada ya Kibali cha Kielektroniki cha Kusafiri (ETA) na ada za kuingia katika hifadhi za taifa za wanyamapori iliyooongezwa hivi majuzi.
Mtaalamu wa utalii, Bw Tony Kirimi alisema watalii wengi tayari huingia nchini wakiwa na bima kamili ya afya walizonunua nchi zao.
“Hivyo basi hakuna sababu ya kuwalazimisha kununua nyingine nchini Kenya. Tulikubali ada ya ETA, ada za kuingia kwenye mbuga zilipandishwa na sasa tunaanzisha bima ya afya ya lazima ambayo ni ghali zaidi kuliko ilivyo katika baadhi ya mataifa ya Ulaya. Kulikuwa na maana gani ya kuondoa visa halafu tuanzishe gharama nyingine?” aliuliza.
Aliongeza kuwa Kenya bado inapambana kuvutia watalii na kujenga jina lake kama kitovu kikuu cha utalii duniani na hivyo haipaswi kuweka sera zitakazozuia watalii kuchagua mataifa mengine.
Wadau wa utalii pia wanaitaka serikali kufafanua ikiwa bima za afya ambazo watalii tayari wanazosafiri nazo kutoka mataifa yao zitatambuliwa, kiwango cha malipo kitakachotozwa na kampuni zitakazoruhusiwa kutoa huduma hiyo.
Bw Mohammed Hersi ambaye ni mtaalamu wa utalii alisema sera hiyo itaongeza gharama kwa watalii.
“Mtalii analipia bima akiwa kwao kabla ya kuja Kenya, halafu analazimishwa kununua nyingine hapa. Je, ingekuwaje kama kila nchi zingekuwa na sharti kama hilo? Swali si kama ni dola kumi au mia moja, ikiwa malipo hayo hayana msingi, basi ni mzigo usiofaa,” alisema kwenye mjadala katika mtandao wa Facebook.
Wadau hao sasa wanataka serikali kusitisha utekelezaji wa sera hiyo na kuanza kufanya mashauriano kati ya Wizara za Afya, Utalii, kampuni za bima na wadau wa sekta hiyo.
Mjadala huo umeibuka wakati ambapo sekta ya utalii inaendelea kunoga. Hii ni baada ya Kenya kunakili idadi kubwa ya watalii wanaozuru mbuga za kitaifa za Wanyama porini.
Kulingana na shirika la huduma ya Wanyamapori nchini (KWS), hifadhi za taifa zimepokea zaidi ya watalii milioni 3.5 huu mwaka ikilinganishwa na milioni mbili mwaka jana.
Hata hivyo asilimia 60 ya wageni hao ni watalii wa humu nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa KWS, Prof Erustus Kanga, alisema mapato ya shirika hilo pia imeongezeka kutoka Sh2.9 bilioni mwaka 2022 alipochukua mamlaka hadi Sh10.5 bilioni mwaka huu kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watalii na uhamasisho.
Hata hivyo, wadau wa sekta ya utalii wanaonya kuwa gharama hiyo mpya ya bima ya afya kwa wageni itaathiri utalii.