Habari

Pacha waliokutanishwa baada ya miaka 20 waomba msaada

Na STEVE KETER NA JARED NYATAYA August 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

DADA mapacha ambao kuunganishwa kwao baada ya kutenganishwa walipozaliwa kulivutia Kenya 2019 wamefichua kuwa furaha ya kupatana kuliambatana na miaka ya mateso kisaikolojia, hali iliyowalazimu kuomba usaidizi kutoka kwa wataalamu wa ushauri nasaha na hisia.

Sharon Mathias na Melon Lutenyo, almaarufu kama “Mapacha wa Kakamega,” walitoa ombi hilo Jumamosi wakati wa sherehe za kuadhimisha Sikukuu ya Kimataifa ya Mapacha zilizoandaliwa Eldoret, Kaunti ya Uasin Gishu.

Siku hiyo walijiunga na mapacha kadhaa kusherehekea sikukuu hiyo inayoadhimishwa wiki ya kwanza ya Agosti kila mwaka.

Huku mapacha wengi wakitumia maisha yao kuimarisha uhusiano ulioanzia tumboni na kuboreshwa kupitia matukio waliyoshiriki utotoni, Sharon na Melon walilazimika kujenga maisha yao kutoka mwanzo baada ya kugundua walitenganishwa walipozaliwa.

“Nilikua na Mevis Imbaya kama pacha wangu tusiyefanana, kabla ya kugundua karibu miaka 20 baadaye kwamba nina pacha tunayefanana, ambaye ni Sharon. Ingawa Sharon ni dada yangu kibayolojia, ninamwelewa Mevis zaidi kwa sababu tulishiriki utoto pamoja. Kusawazisha uhusiano kati ya wawili hao ni mapambano kila siku,” alisema Melon.

Kabla ya ugunduzi huo kukumba taifa, Melon aliishi karibu miongo miwili akiamini Mevis Imbaya ni pacha wake wasiyefanana baada ya kulelewa pamoja katika eneo la Furfural, Kakamega.

Kila kitu kilibadilika 2019 wakati Melon na Sharon waliunganishwa kupitia mtandao wa kijamii.

Kufanana kwao kulivutia umma pakubwa na kusababisha vipimo vya DNA vilivyothibitisha ni mapacha wanaofanana.

Vipimo vilevile viliashiria wawili hao walibadlishwa kwa bahati mbaya walipozaliwa katika Hospitali Kuu ya Kakamega 1999.

Kwa Sharon, uvumbuzi huo ulisambaratisha kila kitu alichojua kuhusu utambulisho wako.

Akiwa amelelewa Nairobi na kuamini ni binti wa pekee na kitindamimba katika familia iliyomlea, vipimo vya DNA baadaye vilibaini kuwa mwanamke aliyeamini daima kuwa mama yake, kibiolojia ni mama yake Mevis.

Anasema ugunduzi huo uliashiria mwanzo wa safari yenye uzito kihisia na uchungu ya kujenga upya utambuisho wake, kubainisha mahusiano kifamilia na kujifunza jinsi ya kutoka familia mbili kwa wakati mmoja.