Makala

Umiliki wa nyumba bado changamoto licha ya miradi kadhaa ya ujenzi wa nyumba za bei nafuu

Na WINNIE ONYANDO August 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUKU ndoto ya kumiliki nyumba ikiendelea kuwa ngumu kwa maelfu ya Wakenya kutokana na kupanda kwa gharama za maisha, wawekezaji wanaendelea kutafuta njia za kuongeza idadi ya nyumba zinazopatikana sokoni.

Haya yanajiri huku serikali ikiendelea kuwekeza mabilioni katika mradi wa ujenzi wa nyumba za bei nafuu.

Ili kuchangia maendeleo hayo, kampuni ya International Housing Solutions (IHS) Kenya imezindua mradi wa nyumba wenye thamani ya Sh1 bilioni katika eneo la Tilisi, Kaunti ya Kiambu, unaolenga kujenga nyumba 240 kwa familia za kipato cha kati.

Uzinduzi huo unafanyika wakati Kenya ikiendelea kukabiliwa na uhaba mkubwa wa nyumba, hali inayochochewa na ongezeko la watu mijini, kuongezeka kw aidadi ya watu na mahitaji makubwa ya makazi bora.

Kwa miaka mingi, Wakenya wengi wamekuwa wakilalamikia gharama kubwa za nyumba katika miji mikubwa kama Nairobi, huku wengi wakilazimika kuendelea kuishi katika nyumba za kupanga kutokana na ugumu wa kupata mikopo ya nyumba na bei ya juu ya ardhi.

Mkurugenzi Mkuu wa IHS Kenya, Bw Kioi Wambaa, alisema kampuni hiyo inalenga si tu kujenga nyumba bali pia kuunda jamii endelevu ambazo zitawanufaisha wakazi kwa muda mrefu.

“Makazi yana mchango mkubwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Tunataka kujenga mazingira ambayo familia zinaweza kustawi huku uwekezaji wao ukiendelea kupata thamani kwa miaka mingi ijayo,” alisema.

Mkurugenzi Mkuu wa IHS Kenya, Bw Kioi Wambaa akizindua mradi w aujenzi wa nyumba eneo la Tilisi, Kaunti ya Kiambu. PICHA|MAKTABA

Kulingana na kampuni hiyo, mradi huo pia unatarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia nafasi za ajira wakati wa ujenzi, pamoja na kuimarisha biashara za ndani zinazotoa bidhaa na huduma zinazohitajika katika sekta ya ujenzi.

Mbali na hilo, Muzi Salama imeundwa kwa kuzingatia mbinu za matumizi bora ya nishati na maji ili kupunguza gharama za maisha kwa wakazi wake.

Mradi huo ni wa pili wa IHS Kenya baada ya maendeleo ya Muzi Stawi katika eneo la Garden City, ambalo kampuni hiyo inasema limevutia idadi kubwa ya wapangaji na wanunuzi.

Kupitia mradi huo mpya, kampuni hiyo inalenga kufikisha jumla ya nyumba 3,000 kufikia mwaka wa 2030.

Hata hivyo, wataalamu wa sekta ya nyumba wanasema kwamba ingawa miradi kama hiyo inaweza kusaidia kuongeza idadi ya nyumba sokoni, changamoto ya umiliki wa nyumba bado ipo kutokana na viwango vya juu vya riba, gharama za ujenzi na mapato ya chini kwa wananchi wengi.

Takwimu zinaonyesha kuwa Kenya inakabiliwa na pengo kubwa la makazi, huku mahitaji ya nyumba mpya yakiongezeka kila mwaka.

Serikali na sekta binafsi zimekuwa zikihimizwa kushirikiana ili kuongeza upatikanaji wa nyumba zinazoweza kumilikiwa na wananchi wa kawaida.

Kadri idadi ya watu mijini inavyoendelea kuongezeka, wataalamu wanaamini kuwa uwekezaji wa muda mrefu katika sekta ya makazi utakuwa muhimu katika kupunguza uhaba wa nyumba na kuboresha maisha ya maelfu ya familia za Wakenya.