Gachagua akivutia umati mkubwa Bonde la Ufa, asidhanie hizo ni kura – Cheruiyot
WASHIRIKA wa Rais William Ruto sasa wanasema aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua yuko huru kuzuru Bonde la Ufa Kusini, lakini wakamwonya asichukulie mapokezi atakayopata kama ishara ya uungwaji mkono katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Akizungumza katika Taasisi ya Mafunzo ya Ufundi ya Chepalungu, Kaunti ya Bomet, Kiongozi wa Wengi katika Seneti Aaron Cheruiyot alisema wakazi wa Bonde la Ufa huwapokea viongozi wote bila ubaguzi, lakini bado wanaunga mkono Rais Ruto na chama cha UDA.
“Bw Gachagua anakaribishwa kama kiongozi mwingine yeyote. Sisi ni watu wenye ukarimu, lakini asidhani umati utakaompokea ni kura. Ukarimu wetu usichukuliwe kuwa uungwaji mkono wa kisiasa,” akasema Seneta Cheruiyot.
Alimkumbusha Bw Gachagua kuwa mnamo 2017 muungano wa NASA ulikusanya umati mkubwa Bomet wakati wa kampeni, lakini Rais wa zamani Uhuru Kenyatta ndiye aliyeshinda kwa kura nyingi katika eneo hilo.
Kauli hiyo inajiri huku Bw Gachagua akitangaza mipango ya kuzuru Bonde la Ufa Kusini, akidai wakazi wamekata tamaa kutokana na kile alichosema ni ukosefu wa maendeleo licha ya kumuunga mkono Rais Ruto 2022.
Hata hivyo, Bw Cheruiyot alikanusha madai hayo akisema eneo hilo linaendelea kunufaika na miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo barabara, hospitali, miradi ya maji, taasisi za elimu ya juu na viwanja vya ndege.
Viongozi wengine waliohudhuria mkutano huo walisisitiza kuwa jamii ya Kipsigis itaendelea kumuunga mkono Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027 na kuwataka wakazi kujisajili kama wapigakura mapema.