Baya afichua kilichofanya Aisha Jumwa atimke kutoka UDA
NAIBU kiongozi wa walio wengi katika Bunge la Kitaifa, Bw Owen Baya, amefichua kile alichodai kilimsukuma aliyekuwa Waziri wa Jinsia Aisha Jumwa, kujiondoa katika chama cha United Democratic Alliance (UDA).
Kulingana na Baya, Jumwa alihama baada ya kukosa hakikisho la tikiti ya kuwania ugavana wa Kilifi mwaka 2027.
Kwa mujibu wa Bw Baya, Bi Jumwa alimtafuta Rais William Ruto kupitia ujumbe mfupi wa simu akiomba wakutane ili kujadili hatma yake ya kisiasa na matarajio yake ya kuwania ugavana wa Kilifi.
“Tunangojea atuambie ataenda chama gani, lakini hatutakubali kutumia uongo, machozi na udanganyifu. Siku ya Jumapili, Bi Jumwa alimtumia Rais ujumbe mfupi akiomba kukutana naye. Rais akamwambia ataangalia ratiba yake, kwa sababu amekuwa akimtafuta kwa muda mrefu,” alisema Bw Baya.
Alisema Rais alikubali kukutana naye katika Ikulu siku ya Jumanne, ambapo walifanya mazungumzo kuhusu mustakabali wa kisiasa wa kaunti ya Kilifi.
Kwa mujibu wa Bw Baya, Bi Jumwa alimweleza Rais kuwa hajaridhishwa na jinsi ambavyo, amekuwa akifanya ziara Kilifi akiwa pamoja na Gavana Gideon Mung’aro na viongozi wengine bila kumhusisha, na akaomba ahakikishiwe tikiti ya UDA katika kuwania ugavana mwaka 2027.
“Alimwambia Rais amhakikishie tikiti ya ugavana. Lakini Rais alimwambia kuwa bado ni mapema mno kufanya uamuzi huo na hivyo kuombwa awe na subra,” alisema Bw Baya kwenye mkutano na wanachama wa UDA huko Kilifi.
Baya anadai kuwa Rais alimweleza Bi Jumwa kuwa kutokana na ushirikiano uliopo kati ya UDA na ODM, suala la mgombea wa ugavana wa Kilifi lingeamuliwa kupitia mashauriano ya viongozi wa vyama hivyo.
Mbunge huyo wa Kilifi Kaskazini alisema kuwa Rais alipendekeza kikao kitakachowahusisha viongozi mbalimbali, akiwemo Gavana Mung’aro na viongozi wa ODM akiwemo kinara wake Bw Oburu Odinga, ili kujadili namna ya kupata mgombea mmoja.
Hata hivyo, Bw Baya adai kuwa Bi Jumwa alisisitiza kuwa anahitaji hakikisho la tikiti hiyo, na pia akataka Rais ampigie simu Bw Baya ili ashurutishwe kumuunga mkono.
“Rais alimwambia avumilie kidogo kwa sababu muda wa kufanya maamuzi haujafika. Pia alimweleza kuwa mgombea wa UDA ataamuliwa kwa kuzingatia maoni kuhusu nani ana nafasi bora ya kushinda. Atakayeshindwa angepewa nafasi nyingine ya uongozi kama uwaziri au useneta,” alifichua Bw Baya.
Bw Baya alimshutumu Bi Jumwa kwa kumwekea Rais masharti.
“Unawezaje kumpa Rais masharti? Rais alimwambia kama hawezi kusubiri kwa miezi michache iliyobaki, basi yuko huru kufanya uamuzi,” alisema.
Tangu alipotangaza kujiondoa UDA, viongozi wa vyama mbalimbali na miungano ya kisiasa wamekuwa wakimtembelea katika makazi yake ya Kakuyuni, Malindi, wakimshawishi ajiunge nao.
Miongoni mwa waliomtembelea ni kinara wa vuguvugu la Linda Mwananchi, Bw James Orengo, pamoja na viongozi kutoka vyama vya Wiper na Jubilee.
“Munajua nimeshahama chama cha UDA, na sasa nimefungua milango ya mashauriano na watu wa Kilifi, pwani na taifa zima. Kwa sasa sitaongea, nitapasua mbarika kadri tunavyoendelea lakini niko katika kipindi cha mazungumzo, nimepata fursa ya kuzungumza na kinara wa Wiper Bw Kalonzo Musyoka na atakuja Malindi na tutafanya mkutano mkubwa sana,” alisema Bi Jumwa.
Alisema wakazi wa Kilifi wanakandamizwa na kulazimishwa kuchagua gavana wa muungano wa UDA-ODM.
Hata hivyo, Bi Jumwa amesisitiza kuwa bado anaendelea na mashauriano na wananchi pamoja na wadau wa kisiasa kabla ya kutangaza chama atakachotumia kuwania kiti cha ugavana wa Kaunti ya Kilifi katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.