Dimba

Idara ya Usalama, Bodi ya Utalii wazindua ligi ya ‘Panga Boys’ Lamu

Na KALUME KAZUNGU August 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

IDARA ya Usalama kupitia Kitengo cha Polisi wa Watalii (TPU) kwa ushirikiano na Bodi ya Utalii Lamu (LTA), Shirikisho la Kandanda Nchini (FKF), tawi la Lamu, na serikali ya kaunti wamezindua ligi maalum inayolenga kukabiliana na uhalifu wa mapanga na dawa za kulevya miongoni mwa vijana eneo hilo.

Ligi hiyo ya mpira wa miguu iliyozinduliwa Jumatatu inajumuisha vijana wasiozidi umri wa miaka 18.

Jumla ya timu kumi na sita (16) zimeshirikishwa kwenye ngarambe hiyo ya wiki tatu mfululizo.

Vilabu hivyo ni Nyundo FC, Crocodile FC, AC Milan, Swafaa FC, Dragon Fly FC, Al Aman, Kashmir City, Real Madrid FC, Rising Stars, Gen 2, Mararani FC, Lamu Boys FC, Home Boys FC, Al Azhar, Riyadha FC na Ukhtein FC.

Timu zote ni za kisiwa cha Lamu.

Akizungumza kwenye hafla ya kuzindua kiny’anganyiro hicho kwenye uwanja wa Twaif kisiwani Lamu Jumatatu, katibu wa kamati andalizi, ambaye pia ni Mwakilishi wa Vijana katika FKF, Lamu, Bw Athman Farid, maarufu Pirezi, aliwataka vijana kupendana na kuepuka kujiingiza kwenye magenge ya uhalifu na mihadarati.

“Ligi yenyewe imeanzishwa madhumuni yakiwa ni kumaliza uhalifu wa mapanga na kuweka amani. Na ndiyo sababu tukaipa jina ‘Weka Panga Chini, Chukua Mpira-Jenga Amani na Mustakabali wa Vijana’. Tupendane na kudumisha amani tunapocheza,” akasema Bw Farid.

Kauli yake iliungwa mkono na Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii Lamu (LTA) Fridah Njeri, aliyesisitiza kuwa ili Lamu kuvutia wageni zaidi wa kitaifa na kimataifa, lazima amani na utulivu vidumishwe.

“Lamu ni kivutio cha watalii na wageni hawawezi kuvutiwa kuja hapa iwapo usalama unadorora. Tutumie ligi hii kuhubiri amani ili Lamu yetu iwe eneo zuri la wageni kuja na uchumi wetu kuimarika,” akasema Bi Njeri.

Mkurugenzi wa Idara ya Michezo na Vijana wa Kaunti ya Lamu Peter Ndichu, alisema mbali na kukabiliana na mihadarati na ‘Panga Boys,’ kinyang’anyiro kilichozinduliwa pia kinalenga kutambua vipaji vya kandanda miongoni mwa vijana wanaoshiriki ili kuwatafutia nafasi ya kucheza nje ya Lamu.