Habari

Wantam, tutam: Uchaguzi wa urais ulifaa kufanyika Agosti 2026 mahakama yasema

Na BRIAN OCHARO August 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imesema uchaguzi ujao wa urais nchini ulifaa kufanyika Agosti 2026, badala ya 2027, lakini imekataa kuamuru uchaguzi huo uandaliwe mara moja ikisema hatua hiyo inaweza kutumbukiza nchi katika vurugu.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Malindi Mugure Thande alisema Katiba inahitaji uchaguzi wa urais ufanyike Jumanne ya pili ya Agosti katika mwaka wa tano baada ya uchaguzi mkuu uliopita.
Jaji huyo alisema Ibara ya 136(2)(a) ya Katiba inataka uchaguzi huo ufanyike katika mwaka wa tano na si baada ya mwaka huo kukamilika.
Alisema mwaka wa tano baada ya uchaguzi wa Agosti 9, 2022 ulianza Agosti 9, 2026.
“Kufanya uchaguzi ujao wa urais katika tarehe nyingine yoyote isipokuwa Jumanne ya pili ya Agosti 2026 kutakiuka Katiba,” Jaji Thande alisema.
Hata hivyo, mahakama ilisimamisha utekelezaji wa uamuzi huo hadi baada ya uchaguzi mkuu ujao.
Hatua hiyo inamaanisha kuwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) haijaamrishwa kuandaa uchaguzi wa urais mwezi huu wa Agosti.
Walalamishi katika kesi hiyo, Dkt Owiso Owiso, Khelef Khalifa na Ashioya Biko, walitaka mahakama itoe uamuzi kuhusu tarehe sahihi ya uchaguzi na pia iamuru IEBC kufanya uchaguzi huo Agosti 11, 2026.
Jaji Thande alikataa ombi la kuamuru uchaguzi ufanyike mara moja.
Alisema kesi hiyo iliwasilishwa Oktoba 2025 wakati maandalizi ya uchaguzi wa 2027 yalikuwa tayari yameanza.
Alisema IEBC, wagombea watarajiwa na Wakenya kwa ujumla walikuwa tayari wamejiandaa kwa uchaguzi wa Agosti 2027.
“Kuamuru tume ya uchaguzi kuandaa uchaguzi wa urais Agosti 2026 kutakuwa kutoa amri ambayo haiwezekani kutekelezwa kwa njia ya kiutendaji,” alisema.
Jaji huyo aliongeza kuwa hatua kama hiyo inaweza kuingiza nchi katika machafuko. Mahakama ilisema ililazimika kusawazisha utekelezaji wa Katiba na tahadhari ya kimahakama ili kuepuka kusababisha “vurugu kubwa kitaifa ambazo haziwezi kudhibitiwa”. Mzozo huo ulitokana na tafsiri ya Ibara ya 136(2)(a), inayoweka wakati wa kufanyika kwa uchaguzi wa urais.
Walalamishi walidai kuwa mwaka wa tano baada ya uchaguzi wa Agosti 9, 2022 ulianza Agosti 9, 2026 na kumalizika Agosti 8, 2027. Kwa hesabu hiyo, walisema Jumanne ya pili ya Agosti 2026, ambayo ni Agosti 11, ndiyo tarehe iliyowekwa na Katiba kwa uchaguzi.
Walitegemea pia Ibara ya 259(5)(c), inayoweka namna vipindi vinavyotajwa kwa miaka vinavyopaswa kuhesabiwa.
Walalamishi walitaja uchaguzi wa 2013 na 2017 kama mifano ya kuonyesha kuwa Katiba haimpi rais haki ya lazima ya kutawala kwa miaka mitano kamili iwapo kufanya hivyo kutapingana na tarehe iliyowekwa kikatiba ya uchaguzi.
Jaji Thande pia alisema ratiba ya uchaguzi iliyowekwa na Katiba ina uzito kuliko dhana kwamba rais lazima atumikie miaka mitano kamili.
Alisema IEBC inaposhindwa kutekeleza wajibu wake wa kikatiba, mahakama inaweza kuingilia kati.
Hata hivyo, mahakama ilisitisha utekelezaji wa uamuzi kwamba uchaguzi utakaofanyika nje ya Agosti 2026 utakuwa batili hadi baada ya uchaguzi mkuu ujao.
Hii ina maana kuwa ingawa mahakama imesema tarehe inayofaa kikatiba ilikuwa Agosti 2026, haijaamuru Kenya kufanya uchaguzi wa urais mwezi huo.
Mahakama pia ilisema muhula wa rais si miaka mitano chini ya Ibara ya 136(2)(a), na kwamba, Ibara ya 142 au kifungu kingine chochote cha Katiba hakimpi rais muhula wa miaka mitano.
Kesi hiyo iliwasilishwa kupitia kampuni ya mawakili ya Otieno Ogola & Company Advocates na Osundwa & Company Advocates.
Miongoni mwa waliotajwa kuwa wahusika wenye maslahi katika kesi hiyo ni Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), Katiba Institute, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, UDA, aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga, mwanaharakati Okiya Omtatah, mwanasiasa Jimi Wanjigi, aliyekuwa Waziri Fred Matiang’i na Kenya Human Rights Commission.