Habari za Kitaifa

Kanja aonya makamanda wa polisi kuhusu uhuni

Na STEVE OTIENO August 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

INSPEKTA Jenerali wa Polisi, Douglas Kanja ametoa onyo kali kwa maafisa wa polisi na makamanda wao kwamba, watawajibishwa binafsi kwa uhalifu unaotokea katika maeneo yao iwapo uzembe wao au usimamizi hafifu utachangia matukio hayo.

Akihutubia makamanda wakuu wa polisi kutoka sehemu mbalimbali za nchi katika Chuo cha Kitaifa cha Uongozi wa Polisi, Ngong, Jumatano, Bw Kanja alisema viongozi wa polisi hawawezi tena kujitenga na vitendo vya uhalifu vinavyofanyika chini ya usimamizi wao.

Alisema makamanda lazima wahakikishe wanatoa uongozi na usimamizi madhubuti kwa maafisa walio chini yao, akionya kuwa wale watakaoshindwa kuchukua hatua dhidi ya wahalifu wako hatarini kupoteza nyadhifa zao.

“Kamanda yeyote katika ngazi yoyote atakayepatikana akivumilia uhuni au kushindwa kuchukua hatua madhubuti dhidi ya wahalifu atawajibishwa kwa kutotekeleza majukumu yake,” alisema Bw Kanja.

Onyo hilo linajiri huku Huduma ya Kitaifa ya Polisi ikiendelea kujiandaa kwa kipindi cha shughuli za uchaguzi.

Inspekta Jenerali aliwaagiza makamanda kuvunja makundi ya wahalifu na magenge ya wahuni yanayoweza kutumiwa kuvuruga shughuli za kisiasa au kuwatisha wananchi nchi inapoelekea uchaguzi mkuu mwaka ujao.