Makala

Mkenya apokea Sh103m Amerika kukuza ‘managu’

Na DAVID MONDA August 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ARI ya Dkt Truphena Choti, Mkenya anayeishi Amerika, ya kulima mboga za kienyeji za Kiafrika imepigwa jeki baada ya mradi wake kupata ufadhili wa Sh103 milioni.

Fedha hizo zitatumika kukuza biashara yake ya kulima na kusambaza mboga kama kunde, managu, terere, mchicha na mrenda kwa watumiaji nchini Amerika, wengi wao wakiwa Waafrika wanaoishi ughaibuni.

Seneta wa Maryland Chris Van Hollen alimkabidhi Dkt Choti hundi hiyo rasmi Jumatatu, ishara ya kuungwa mkono kwa mradi wake unaolenga kuboresha lishe na upatikanaji wa chakula salama.

Dkt Choti, ambaye ana taaluma ya sheria, alianza kupenda maisha yenye afya na lishe bora kupitia shughuli za kijamii.

Bustani yake ya jamii ilianza kwa kulima vyakula alivyozoea nchini Kenya, ikiwemo viazi vitamu na Sukuma wiki.

Mradi huo, unaojulikana kama AfriThrive Community Food Center, ulianza baada ya Waafrika wengi kuonyesha kuvutiwa na bustani yake.

Kwa sasa unahudumia takriban watu 20,000 kila mwaka.

Dkt Choti alisema malezi yake nchini Kenya, hasa Kisii, yalichangia pakubwa kuibua shauku ya kulima vyakula alivyokua akila.

“Kwetu, utoshelevu wa chakula si kuwapa watu kitu cha kula pekee. Tunataka familia zipate vyakula wanavyojua, wanavyofurahia na vinavyowakumbusha nyumbani,” alisema.

Alisema alipohamia Amerika alikosa mboga alizokua akila Kenya, hasa managu na saga.

“Nilipata kipande kidogo cha ardhi karibu na nyumbani kwangu, ndipo upande wa Kisii ndani yangu ukajiuliza, ‘Kwa nini usilime saga yako mwenyewe?’ Nilifanya hivyo,” alisema.

Dkt Choti ana uzoefu wa karibu miongo miwili katika maendeleo ya kimataifa. Anasema uzoefu huo ulimsaidia kuona kilimo cha mboga hizo kama zaidi ya kutafuta ladha ya nyumbani.

“Bustani nilipanda mbegu, lakini uzoefu wangu wa maendeleo ulinisaidia kuona picha kubwa. Bustani hiyo ndogo hatimaye ikawa AfriThrive,” alisema.

Ufadhili huo utatumika kwanza kukarabati na kuendeleza kituo cha AfriThrive huko Essex.

Kituo hicho kitawekwa vifaa vya kuhifadhi chakula kwa baridi, maeneo ya kuandaa chakula na vifaa vingine vya kuhifadhi na kusambaza chakula salama.

Dkt Choti anasema hatua hiyo itawezesha mradi kutoa huduma mwaka mzima.

Kwa malengo ya muda mrefu, anataka mradi huo kusaidia jamii kuelewa umuhimu wa lishe bora na kuzuia magonjwa yanayohusishwa na lishe duni.

Anasema elimu ya lishe pekee haitoshi ikiwa vyakula bora havipatikani au wengi hawamudu gharama yake.

“Watu wanahitaji maarifa na chakula mezani,” alisema.

Kwa Dkt Choti, mboga za kienyeji pia ni alama ya utamaduni.

“Nilikulia maeneo ya mashambani Kisii, Kenya, ambako tulilima vyakula vingi tulivyokula. Kilimo kimekuwa sehemu ya maisha yangu,” alisema.

Leo, anaongoza AfriThrive kama mkurugenzi mkuu, lakini Jumapili bado ni siku yake ya shamba.

Akiangalia zaidi ya ekari tano zilizo chini ya kilimo cha managu na saga, anasema anakumbushwa utoto wake, familia na mila.

“Haijalishi niko mbali kiasi gani kutoka Kisii, udongo bado hunirudisha nyumbani,” alisema.

Dkt Choti anasema lengo lake ni kuona AfriThrive ikiwa zaidi ya kituo cha kusambaza chakula.

Anataka kuanzisha mipango inayohusisha chakula kama tiba, elimu ya lishe, kusaidia wakulima wa eneo hilo, vijana na familia, huku akiimarisha uhusiano kati ya chakula na afya.

Kilichoanza na mama mmoja aliyetafuta saga, sasa kimekua kuwa mradi unaolenga kuwafikia maelfu ya familia.

“Tunajenga mahali ambapo maelfu ya familia zinaweza kupata chakula bora, heshima na ladha kidogo ya nyumbani,” alisema.