Seneti yapinga uamuzi wa mahakama kuwa ilikiuka haki za Gachagua
SENETI imewasilisha rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu kwamba maseneta walikiuka haki ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ya kusikilizwa kwa haki wakati wa mchakato wa kumtimua mamlakani.
Seneti pia inapinga fidia ya Sh50 milioni ambayo Mahakama Kuu ilimpa Gachagua kwa ukiukaji huo wa haki zake.
Rufaa hiyo iliwasilishwa mwezi mmoja baada ya Gachagua mwenyewe kukata rufaa kupinga sehemu kubwa ya uamuzi wa Mahakama Kuu, ikiwemo uamuzi uliothibitisha kutimuliwa kwake na kuidhinisha Profesa Kithure Kindiki kuwa mrithi wake.
Hata hivyo, Gachagua hakupinga sehemu ya uamuzi iliyosema haki zake zilikiukwa wala fidia ya Sh50 milioni.
Seneti, kupitia Spika wake na Seneti yenyewe, inalenga kubatilisha sehemu za uamuzi wa Juni 8 zilizowalaumu maseneta kwa kukataa ombi la kuahirishwa kwa kikao cha mchakato wa kumtimua Gachagua na kuamuru alipwe fidia.
Katika hati yake ya rufaa, Seneti inataka Mahakama ya Rufaa ibatilishe au ibadilishe maagizo hayo pamoja na kuamuru gharama ya kesi ilipwe.
Seneti inasema majaji walikosea walipoamua kwamba uamuzi wake wa kukataa kuahirisha mchakato huo ulikiuka haki ya Gachagua ya kusikilizwa kwa haki.
Inasema majaji hawakutathmini ipasavyo masharti ya Katiba katika Ibara ya 47 na 50 na hawakutambua kwamba Seneti ilitumia mamlaka yake ya kufanya uamuzi kuhusu ombi hilo.
Seneti pia inasema majaji walikosea baada ya kukiri kwamba Gachagua alipewa nafasi ya kujitetea, lakini baadaye akawalaumu maseneta kwa kuendelea na mchakato huo baada ya yeye kutofika.
Kwa mujibu wa Seneti, Gachagua alipewa muda zaidi kwa ombi la mawakili wake na Bunge lilikuwa na wajibu wa kukamilisha mchakato wa kumtimua bila kuchelewa.
Seneti pia inawashutumu majaji kwa “kunyakua mamlaka ya kufanya uamuzi” ya Seneti na kutumia tathmini yao wenyewe kuamua iwapo ombi la kuahirisha kikao lilipaswa kukubaliwa.
Hati hiyo inasema ombi la kuahirisha mchakato liliwasilishwa kwa kura na likakataliwa baada ya maseneta kuzingatia mazingira yaliyokuwepo wakati huo.
Seneti pia inapinga uamuzi kwamba kutokuwepo kwa Gachagua kulihalalishwa na ugonjwa.
Inasema hakuna ushahidi uliowasilishwa mbele yake wakati huo kuthibitisha kwamba alikuwa mgonjwa.
“Majaji walikosea kisheria na kimantiki walipoamua kwamba kutokuwepo kwa Gachagua kulihalalishwa kwa sababu ya ugonjwa, licha ya kwamba hakuna ushahidi uliowasilishwa mbele ya Seneti wakati huo kuthibitisha ugonjwa huo uliodaiwa,” inasema rufaa hiyo.
Seneti sasa inataka Mahakama ya Rufaa ibatilishe uamuzi kwamba haki za Gachagua za kusikilizwa kwa haki zilikiukwa na pia iondoe agizo la kulipa Sh50 milioni.
Mzozo huo ulitokana na mchakato wa kumtimua Gachagua uliofanyika Oktoba 2024 baada ya Mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse kuwasilisha hoja iliyokuwa na malalamishi 11 dhidi yake.
Bunge la Kitaifa liliidhinisha hoja hiyo na kuiwasilisha Seneti, ambayo ilithibitisha mashtaka matano kabla ya kumwondoa Gachagua afisini.
Gachagua na watu wengine baadaye walipinga mchakato huo, wakidai kwamba haukuhusisha ushiriki wa kutosha wa umma, kulikuwa na upendeleo, taratibu za Bunge zilikiuka Katiba na haki zake zilikiukwa.
Mahakama Kuu ilikataa malalamishi yao mengi na kuthibitisha kutimuliwa kwake, pamoja na uteuzi na kuidhinishwa kwa Profesa Kindiki kuwa Naibu Rais.
Hata hivyo, majaji walipata kasoro katika namna Seneti ilivyoshughulikia utetezi wa Gachagua.
Walibaini kuwa Seneti iliendelea na mchakato huo baada ya Gachagua kuugua kabla hajatoa ushahidi mwenyewe.