Makala

Ghasia za Homa Bay zazua kumbukumbu ya ubabe wa Raila-Orengo miaka ya 90’s

Na CECIL ODONGO August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VURUGU zilizoshuhudiwa katika mikutano ya Linda Mwananchi Homa Bay mwishoni mwa wiki zimeibua tena kumbukumbu za migogoro mikali ya kisiasa iliyotikisa Luo Nyanza baada ya kifo cha Jaramogi Oginga Odinga, mwanasiasa mashuhuri wa eneo hilo.

Kwa sasa, viongozi wa Linda Mwananchi, kundi lililojitenga na ODM, wanakabiliana vikali na mrengo unaoongozwa na Seneta wa Siaya Dkt Oburu Oginga.

Linda Mwananchi inaongozwa na Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi East Babu Owino.

Kiini cha mzozo huo ni msimamo kuhusu uchaguzi wa 2027.

Mrengo wa Dkt Oburu unaunga mkono kuchaguliwa tena kwa Rais William Ruto, huku upande wa Bw Orengo ukitaka ODM kusimamisha mgombea wake wa urais.

Bw Orengo na washirika wake pia wanamlaumu Rais Ruto kwa kuchangia migawanyiko ndani ya ODM.

Kifo cha Raila Odinga kimeacha pengo kubwa la kisiasa Nyanza, huku makundi mbalimbali yakijitokeza kuwania ushawishi katika eneo hilo.

Vurugu za Homa Bay zimewakumbusha wengi tukio la Aprili 24, 1999, wakati uhasama kati ya Raila na Orengo ulifikia kilele katika harambee Ugunja, wakati huo ikiwa sehemu ya eneobunge la Ugenya.

Raila, aliyekuwa akiongoza NDP, na Orengo, aliyekuwa mbunge wa Ugenya, walikuwa wameingia katika mzozo mkali wa kisiasa.

Raila aliwasili kwenye harambee akiwa amevalia agbada ya Nigeria na kuandamana na vijana waliokuwa wakimshangilia kwa kaulimbiu yake ya kampeni “Amollo Tinga”.

Bw Orengo naye aliwasili na kundi la vijana, hali iliyosababisha makabiliano na hatimaye vurugu.

Polisi walilazimika kutumia vitoa machozi na mbwa wa kunusa kuwatenganisha vijana hao.

Bw Orengo alilazimika kukimbilia katika shamba la miti ambako alimshambulia Raila kwa madai ya kuwaleta watu kutoka nje ya Ugenya.

“Magari mengi yalikuja Ugenya, malori yaliyojaa, matatu na watu hao hawatoki Ugenya,” akasema.

Raila naye alijibu kwa kuuliza ni nani aliyemwalika Bw Orengo katika hafla hiyo.

“Ni nani aliyesema naye na kumwalika katika hafla hii? Aliulizwa kama jina lake lingewekwa kwenye kadi ya mwaliko lakini akasema atafikiria,” alisema Raila.

Mwaka huo huo, Raila pia alikabiliwa na upinzani mkali Kisumu kutoka kwa aliyekuwa Meya Akinyi Oile, mshirika wa kisiasa wa Rais wa zamani Daniel Moi.

Uhasama wa Mabw Orengo na Raila ulianza baada ya kifo cha Jaramogi mwaka 1994 wakati wa uchaguzi wa naibu mwenyekiti wa Ford Kenya.

Bw Orengo alishinda kwa kura moja, hatua iliyomkasirisha Raila na kumfanya kumpinga katika kinyang’anyiro cha uongozi wa chama.

Mnamo Machi 18, 1995, uchaguzi wa uongozi wa Ford Kenya katika Uwanja wa Thika uligeuka kuwa vurugu, huku jaribio la kutaka kumuua Raila likiripotiwa.

Leo, historia hiyo inaonekana kujirudia, lakini mara hii bila Raila. Bw Orengo anakabiliana na Dkt Oburu katika vita vya kuwania ushawishi wa kisiasa wa jamii ya Luo.

Upande wa Orengo unaungwa mkono na Babu Owino na Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi, huku Dkt Oburu akiungwa mkono na Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga na Mawaziri Opiyo Wandayi na John Mbadi.

Mbunge wa Suba Kaskazini Millie Odhiambo na Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Kisumu Ruth Odinga nao wana msimamo vuguvugu na hawajaonyesha upande wanaounga mkono.