Habari za Kitaifa

Wahuni walilipwa Sh4,000 kwa siku, mkutano ulifanywa nyumbani kwa mwanasiasa mashuhuri -Ufichuzi

Na WAANDISHI WETU August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VURUGU zilizotokea Homa Bay Jumapili wakati wa mikutano ya kundi la Linda Mwananchi huenda zilipangwa siku kadhaa kabla, huku wanasiasa wakidaiwa kuwahamasisha vijana na kuunda mtandao wa kuratibu uvamizi.

Duru kutoka kwa polisi na mahojiano na baadhi ya vijana waliohusika vilifichua kuwa mkutano wa kwanza ulifanyika Agosti 2 nyumbani kwa mwanasiasa mashuhuri, muda mfupi baada ya hafla ya kumkaribisha Mbunge wa Mwakilishi wa Kike wa Homa Bay, Joyce Osogo.

Vijana hao walidaiwa kuagizwa kumzuia Gavana wa Siaya James Orengo pamoja na kikosi cha Linda Mwananchi, inayojumuisha Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, kufanya mikutano katika kaunti hiyo.

Inadaiwa kila kijana aliyehusika katika fujo hizo alilipwa kati ya Sh2,000 na Sh4,000. Wale waliolipwa Sh4,000 walidaiwa kusafirishwa kutoka kaunti jirani ya Migori.

Siku moja kabla ya mikutano hiyo, vijana walifanya mkutano mwingine katika eneo la Lo Rateng, uliokuwa umeandaliwa na Mbunge wa Homa Bay Mjini Peter Kaluma.

Katika video iliyosambazwa mitandaoni, Bw Kaluma aliwataka wafuasi wake kuwafukuza wanachama wa kundi pinzani aliowatuhumu kuingilia shughuli za ODM.

Alisema: “Tunatoa amri sasa kwamba yeyote anayesema muhula mmoja afukuzwe.”

Pia aliwataka wafuasi wake kuwatafuta wanachama wa Linda Mwananchi katika hoteli na maeneo mengine ya kulala na kuwafukuza.

Muda mfupi baadaye, ripoti za uvamizi zilianza kuibuka katika maeneo mbalimbali ya Homa Bay. Vijana waliokuwa kwenye pikipiki walionekana wakiwa na panga, marungu na silaha nyingine hatari.

Katika Hoteli ya Homa Bay Tourist, vijana waliingia kwa nguvu, wakawafukuza wageni na kuwashambulia wafanyakazi. Walivamia vyumba 21 na kuiba magodoro na televisheni.

Pia waliharibu kanda za CCTV ili kuzuia kurekodiwa kwa matukio yaliyofuata.

Baada ya hapo, vijana hao waliagizwa kukutana katika kituo cha mabasi cha Homa Bay saa 10 alfajiri Jumapili na kuweka vizuizi barabarani ili kuzuia watu wanaohusishwa na Linda Mwananchi.

Mawe na vitu vingine vilitumiwa kuziba barabara, hali iliyowalazimisha wakazi kubaki nyumbani huku baadhi ya wafanyabiashara wakishindwa kufika sokoni.

Mmoja wa vijana waliozungumza na Taifa Leo alisema maagizo yalipitishwa kupitia simu kutoka kwa wanasiasa na wahamasishaji wa vijana.

Alidai baadhi ya vijana hutumiwa kama walinzi binafsi wa wanasiasa na hupewa silaha kabla ya maandamano.

Kamishina wa Kaunti ya Homa Bay Ronald Mwiwawi alisema baadhi ya vijana walikuwa wameunganisha panga mbili kwa kuzichomelea ili kutengeneza silaha ndefu zaidi.

Vurugu ziliongezeka msafara wa Bw Orengo ulipokaribia Homa Bay. Msafara huo, uliokuwa na Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, ulizuiwa Ndhiwa na mzunguko wa Kodoyo.

Polisi walitumia gesi ya kutoa machozi kuwatawanya vijana waliokuwa wamefunga barabara.

Baadhi ya vijana waliokuwa katika msafara wa Linda Mwananchi pia walihusika katika kuwatawanya wapinzani. Magari kadhaa yalipigwa mawe na mengine kugongana.

Baada ya mikutano ya Nyandiwa na Sindo, msafara ulipokuwa ukirejea Homa Bay Mjini, mapigano mengine yalizuka karibu na mzunguko wa Kodoyo.

Mmoja wa vijana aliyeokolewa na wanahabari wa Taifa Leo alikuwa na majeraha makubwa shingoni, mkononi na mgongoni. Alidai alikuwa ndani ya gari lililochomwa moto.

Mtu mmoja anayetajwa kama Abdi alidaiwa kuwa kiungo muhimu kati ya wanasiasa na vijana. Duru zilisema Abdi, anayetajwa kuwa kiongozi wa vijana wa ODM, ana ushawishi mkubwa na hujulikana kwa jina la “Kamanda.”

Duru ziliarifu kuwa Abdi hupokea simu kutoka kwa viongozi kabla ya kuwasiliana na vijana kutoka maeneo ya Shauri Yako, Sophia, Misita na Got Rabuor.

Kwa vijana wengi wasio na ajira, ahadi ya pesa za haraka imekuwa kivutio kikubwa. Baadhi yao walidaiwa kulipwa Sh2,000 baada ya kushiriki vurugu.

Vurugu hizo hata ziliingia katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Kaunti ya Homa Bay, ambako vijana walijaribu kuingia baada ya kusikia kuwa baadhi ya waliojeruhiwa walikuwa wakipatiwa matibabu.

Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Vincent Oduor, alisema polisi waliitwa kusaidia kudhibiti hali hiyo.

Wakati huo huo, ushahidi uliokusanywa ulionyesha kuwa upande wa Linda Mwananchi pia ulikuwa umejiandaa kwa uwezekano wa makabiliano.

Duru kutoka kundi hilo zilisema baadhi ya wagombea waliokuwa katika msafara walikuwa na leseni za kumiliki bunduki na walikuwa wameandaa walinzi wenye silaha.

Polisi walikamata watu 15 waliodaiwa kuhusishwa na Linda Mwananchi katika Kaunti ya Kisumu na kupata silaha hatari. Watu wengine wawili walikamatwa Migori na panga tano zikapatikana.

Kamanda wa Polisi wa Homa Bay Lawrence Koilem alisema watu wasiopungua 22 walikamatwa kuhusiana na vurugu hizo. Polisi pia walipata bastola aina ya Ceska iliyokuwa na risasi 13.

Vurugu hizo ziliacha watu wawili, akiwemo afisa wa polisi, wakiwa wamefariki, huku wengine kadhaa wakijeruhiwa. Magari sita yalichomwa moto na biashara kadhaa kuporwa.