Hata waliotorokea kanisani walipigwa Homa Bay
KANISA la SDA Lake Victoria Field liligeuka kuwa eneo la vurugu Jumapili baada ya watu waliokuwa wakitoroka makabiliano ya kisiasa Homa Bay kukimbilia humo kutafuta hifadhi.
Kasisi Dan Okumu alisema mlinzi wa kanisa alifungua lango kuruhusu waliokuwa wakitoroka uvamizi kuingia, lakini vijana wenye silaha waliwafuata na kuwashambulia.
“Inajulikana kwamba kanisa ni mahali ambapo watu hukimbilia kupata hifadhi. Hilo ndilo tulilokuwa tunajaribu kufanya,” akasema.
Bw Okumu alisema alishuhudia watu waliokuwa ndani ya gari wakikatwa kwa mapanga. Mwanamke mmoja alifanikiwa kutoroka, lakini dereva alibaki chini akishambuliwa.
Gari hilo lilichomwa moto kwenye lango la kanisa kabla ya vijana kurusha mawe kwenye afisi za SDA, kuvunja madirisha na kuharibu magari.
Mkuu wa SDA Lake Victoria Field, Samson Okwach, alisema baadhi ya wafanyakazi walijeruhiwa na kulaani mashambulizi hayo.
Katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Kaunti ya Homa Bay, watu 46 walitibiwa baada ya vurugu hizo.
Mkurugenzi Mkuu Vincent Oduor alisema wagonjwa saba walikuwa katika hali mbaya, mmoja akahamishwa hadi hospitali ya Jaramogi Oginga Odinga mjini Kisumu.
Polisi mmoja alipigwa kichwani, watu wanne walikuwa na majeraha ya risasi miguuni, huku wengi wakitibiwa majeraha ya mapanga na visu.
“Mwanamke mmoja alifariki baada ya kugongwa na gari lililokuwa likienda kwa kasi,” alisema Dkt Oduor.