Siasa

Eti sijui kusoma? Wewe ndio ulikuwa unanililia ulipopokonywa Wizara ya Ulinzi, Jumwa ajibu Duale

Na CECIL ODONGO August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

ALIYEKUWA Waziri wa Utumishi wa Umma Aisha Jumwa wikendi alimjibu vikali Waziri wa Afya Aden Duale baada ya kutoa madai ya kutokuwa na uwezo wa kusoma na kuelewa stakabadhi za Baraza la Mawaziri walipokuwa serikalini.

Bi Jumwa alimshutumu Bw Duale kwa unafiki na kusema matamshi yake yalilenga kumdhalilisha kisiasa. Alisisitiza kuwa alikuwa na uwezo kamili wa kuelewa shughuli za Baraza la Mawaziri.

“Nilikaa nawe katika Baraza la Mawaziri na hakuna siku yoyote ulizungumza nami isipokuwa siku moja,” akasema Bi Jumwa.

Alidai Bw Duale alimkasirikia baada ya kumpeleka mmoja wa magavana wa zamani kumwona Rais William Ruto.

“Siku hiyo ulipozungumza nami ulikuwa na hasira kubwa, ukiniuliza kwa nini nilimpeleka gavana huyo kwa Ruto,” akasema.

Bw Duale alikuwa amemshambulia Bi Jumwa Jumamosi jijini Mombasa, akidai wakati walipokuwa Barazani alikuwa akimsaidia kusoma na kuelewa baadhi ya stakabadhi za serikali.

Alisema mara kadhaa Bi Jumwa alishindwa kueleza baadhi ya masuala yaliyokuwa kwenye hati hizo, hivyo akalazimika kumsaidia.

Bw Duale alitoa matamshi hayo alipokuwa akikosoa uhusiano wa Jumwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua pamoja na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka.

Hata hivyo, Bi Jumwa alimtaka Bw Duale kuacha kujaribu kuamulia Pwani upande wa kisiasa wa kuunga mkono.

“Hutatuamulia Pwani mahali pa kupigia kura. Pwani ina viongozi wake na ikiwa unafikiri Pwani haina kiongozi, mimi niko hapa kwao,” alisema.

Mbunge wa EALA Falhada Iman Dekow pia alilaani matamshi ya Bw Duale, akisema tofauti za kisiasa hazifai kugeuka kuwa vita vya kibinafsi dhidi ya viongozi wanawake.

Alisema kila kiongozi ana haki ya kidemokrasia kuchagua upande wa kisiasa anaounga mkono.