Akili MaliMakala

Alivyopandisha hadhi ya shamba lake kwa kulima pitaya

Na SAMMY WAWERU August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

UNAPOZURU shamba lake, utakaribishwa na mseto wa mimea na mazao japo kinachojitokeza zaidi ni kilimo cha matunda yanayostahili kiangazi na ukame.

Pitaya, maarufu kwa Kiingereza kama dragon fruits, ni matunda yaliyopandisha hadhi ya shamba lake. Si mwingine ila ni Kennedy Macharia, maarufu kama Macha wa Dragon.

“Haijakuwa safari ya leo, jana ama juzi kupandisha hadhi ya shamba langu,” anasema. Kwanza, alitangulia kulitafuta – aitwe mmiki wa ardhi.

Anasimulia kwamba mwaka 2003, yeye na rafiki yake walianza kutafuta kipande cha ardhi huko Joska, Kaunti ya Machakos, ambako wangeweza kuishi na familia zao. Uamuzi huo, hatimaye uliishia kuwa fursa yenye thamani kubwa.

Macharia, ambaye wakati huo alikuwa akifanya kazi za vibarua katika sekta ya ujenzi, alinunua ekari moja kwa Sh600,000. Leo hii, kipande hicho kinakadiriwa kuwa na thamani ya Sh10 milioni na kina shamba la matunda ya dragon.

“Wakati huo ardhi Joska ilikuwa ya bei nafuu kwa sababu ilikuwa bado halijaendelezwa na kukua,” anakumbuka.

Anasema hii leo ni vigumu kupata ekari moja, kwani wawekezaji wa ardhi hununua mashamba makubwa, kuyagawanya kuwa ploti za futi 50 kwa 100 na kuziuza hadi Sh1.3 milioni kila kimoja.

Mipitaya kwenye shamba la Kennedy Macharia, Joska, Machakos. Picha|Sammy Waweru

Akiwa mwasisi wa Kran Farm, ambaye anatoka Kangema, Murang’a, anaeleza kuwa Joska ni eneo kame na nusu-kame (ASAL), ambapo kilimo cha mfumo wa umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa kutumia mifereji (irrigation) au uwekezaji wa ujenzi wa nyumba za kukodisha ndio unaoweza kuleta faida kutokana na uhaba wa maji eneo hilo.

Baada ya kukamilisha kulipa shamba lake na kuhamia huko mwaka 2014, Macharia alianza kilimo cha mahindi, maharagwe, soya, mboga na ufugaji wa kuku, mbuzi na vilevile sungura. “Nilitegemea mvua pekee, jambo lililoniletea hasara wakati wa misimu ya kiangazi na ukame,” anaelezea.

Ukame mbaya wa 2022 hadi 2023 ulimfanya aanze kutafuta zao linaloweza kustahimili athari za mabadiliko ya tabianchi, ukame na kiangazi vikiwemo. Utafiti wake ulimpeleka kwenye matunda ya pitaya, ndiyo dragon, zao linalofanana na kaktasi na ambalo linazidi kupata umaarufu miongoni mwa wakulima na walaji.

Alipotembelea shamba la matunda hayo huko Juja, alivutiwa na uwezo wake wa kustawi katika eneo kame. Pia aligundua kuwa tunda moja linaweza kuuzwa kwa karibu Sh1,000 kulingana na ukubwa na ubora.

Mwaka 2023 alinunua miche 40 kwa Sh850 kila moja. Miche yote ilistawi na kuanza kuzaa baada ya takriban mwaka mmoja.

Leo hii, Macharia ana mipitaya kati ya 700 na 800 kwenye robo ekari, inayozalisha kilo 250 hadi 300 za matunda kwa mwezi, huku nyakati zingine mavuno yakifika kilo 400.

Macharia analenga kuzalisha matunda makubwa yenye uzani wa karibu gramu 500 kila moja. Anatumia samadi kutoka kwa mbuzi na kuku wake kuongeza rutuba ya udongo. Biashara hiyo sasa imebuni ajira kwa vibarua wawili, hususan wakati wa mavuno.

Kennedy Macharia akikagua pitaya kwenye shamba lake Joska, Machakos. Picha|Sammy Waweru

Soko lake limepanuka kupitia mitandao ya kijamii kama vile Facebook, Instagram, TikTok na YouTube, huku binti yake akihusika pakubwa katika uuzaji wa kidijitali na kusaka taarifa kuhusu mbinu mpya za uzalishaji na mwenendo wa soko. Macharia huuza matunda ya pitaya Nairobi na pia majirani eneo la Joska.

Anasisitiza umuhimu wa kutunza rekodi za biashara na kufuatilia gharama. “Lazima uelewe mahesabu ya kilimo-biashara. Usipohifadhi rekodi na kufuatilia gharama, hutajua biashara inavyoendelea na utakuwa mwenyeji wa hasara,” anasema.

Ili kupunguza gharama, sasa huzalisha miche yake mwenyewe kutoka kwa mimea iliyokomaa. Hali kadhalika, hutumia teknolojia ya matuta yaliyoinuliwa na kufunika udongo kwa mabaki mimea iliyokauka, ikiwemo nyasi, ili kuhifadhi unyevuunyevu na kudhibiti kwekwe dhidi ya kumea.

Isitoshe, amewekeza katika uvunaji wa maji, ikiwa ni pamoja na matangi na bwawa lenye uwezo wa kuhifadhi karibu lita 50,000.

“Uhaba wa maji bado ni changamoto kubwa, lakini matunda ya dragon yana matatizo machache ya magonjwa,” anaelezea. Pia, hupanda Mexican marigold kati ya mistari ya mipitaya ili kufukuza wadudu kwa njia ya kiasili.

Macharia anaamini zao hilo linaweza kusaidia wakulima wa maeneo kame kupata mapato kutoka kwa mashamba madogo.