Kampeni zaanza Nigeria Tinubu akikabiliwa na ushindani mkali anaposaka ‘Tu Tam’
ABUJA, Nigeria:
KAMPENI za uchaguzi wa Januari 2027 Nigeria zilianza Jumatano huku Rais Bola Tinubu akikabiliwa na swali gumu anapowania muhula wa pili hasa kuhusu utendakazi wake.
Wengi wanajiuliza iwapo wananchi wa Nigeria wanaishi maisha bora baada ya zaidi ya mwongo mmoja wa utawala wa chama cha All Progressives Congress (APC).
Tinubu yupo katika kinyang’anyiro dhidi ya aliyekuwa Makamu wa Rais Atiku Abubakar na Peter Obi, ambao wamekita kampeni zao katika masuala ambayo wananchi wanalalamikia hasa ugumu wa maisha na ukosefu wa usalama.
Wapinzani wanadai kuwa miaka karibu 12 ya APC madarakani imeiacha Nigeria, taifa lenye watu wengi zaidi Afrika, likiwa maskini zaidi, lenye madeni mengi na lisilo salama kuliko 2015. Hali ni mbaya zaidi ikilinganishwa na chama hicho kilipoingia mamlakani chini ya aliyekuwa Rais Muhammadu Buhari.
Kwa Tinubu, ambaye baadhi ya wananchi humwita “T-Pain” kutokana na gharama ya juu ya maisha, uchaguzi huo utakuwa kipimo cha iwapo wapiga kura wako tayari kuvumilia maumivu ya muda mfupi kwa matumaini ya kupata nafuu ya muda mrefu.
Asilimia 80 ya raia wa Nigeria wanaamini nchi yao inaongozwa vibaya, huku asilimia 45 wakitaja ugumu wa kiuchumi na ukosefu wa usalama kuwa changamoto zao kuu.
Tinubu amefanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi tangu aingie madarakani. Alifuta ruzuku ya mafuta iliyokuwa ikigharimu serikali fedha nyingi na kushusha thamani ya naira mara mbili.
Hatua hizo zimepongezwa na wawekezaji na wakopeshaji wa kimataifa, lakini pia zimesababisha athari za kiuchumi kwa familia na kuchochea maandamano kutokana na kupanda kwa gharama ya maisha.
Serikali ya Tinubu inasema mageuzi hayo yameimarisha mapato ya serikali na kuongeza imani ya wawekezaji. Hata hivyo, wananchi wengi hupima hali ya uchumi kwa uwezo wao wa kununua chakula na kugharamia mahitaji ya familia.
Mfanyabiashara wa nyama Abdullahi Sani alisema zamani alikuwa akiuza mbuzi sita kwa siku, lakini sasa anahangaika kuuza hata wawili.
Mizigo ya madeni pia imeongezeka.
Usalama nao ni changamoto kubwa kwa Tinubu. Ingawa serikali inasema operesheni za kijeshi zimepunguza mashambulizi na kuwezesha wakulima kurejea mashambani, ghasia, utekaji nyara na ujambazi bado umeenea.
Wapinzani sasa wanatumia hali hiyo kumshambulia Tinubu, wakisema baada ya zaidi ya miaka 10 ya APC madarakani, wananchi wanataka kuona matokeo, si ahadi.
Kwa wapiga kura wengi, uchaguzi huo utahusu maisha, usalama na chakula.
Hata hivyo, mgawanyiko katika upinzani unaweza kumpa Tinubu nafasi ya kubaki madarakani licha ya changamoto zinazokabili uongozi wake.