Akili MaliMakala

Atafanikiwa kuingia kwenye rekodi ya Guinness kwa kufuga mamilioni ya kuku halisi wa kienyeji?

August 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KILOMITA chache kutoka barabara kuu ya Nairobi-Mombasa, katika shamba la Nick Mwendwa eneo la Makindu, Kaunti ya Makueni, unapolizuru utakaribishwa na milio ya maelfu ya kuku halisi wa kienyeji.

Shamba hilo la ekari 100, ambapo ni ekari 10 pekee zimetumika kwa sasa, lina zaidi ya kuku 150,000 wa kienyeji wa umri tofauti.

Kila siku, karibu mayai 2,500 hukusanywa na kuwekwa kwenye mashine za kuatamia mayai na kuangua vifaranga (incubators). “Kila baada ya siku 21, vifaranga huanguliwa ili kupanua mpango wa uzalishaji unaolenga kuongeza idadi ya kuku,” anasema.

Mwendwa, ambaye wengi wanamfahamu kutokana na uongozi wake wa zamani katika Shirikisho la Soka Kenya (FKF), alianza mradi huo miaka mitatu iliyopita akiwa na kuku saba tu wa mama yake. “Nilitenga kuku hao saba na nikaapa kwamba kuanzia siku hiyo tutakuwa tukizalisha kutoka kwao pekee,” anafichua.

Nick Mwendwa akikagua kuku wake. Anahoji analenga kufikisha idadi ya kuku milioni moja hivi karibuni. Picha|Sammy Waweru

Awali, alilenga kuongeza kundi hilo hadi kuku kati ya 7,000 na 15,000. Mama yake alicheka, akimwambia hakuna aliyekuwa na kuku 5,000 wa kienyeji halisi nchini.

Hata hivyo, baada ya kutambua jinsi walivyohitajika sokoni, alibadilisha lengo na kulenga kuku milioni moja. “Baba yangu aliposikia mazungumzo hayo kati yangu na mama, alisema Nairobi imenigeuza kuwa wazimu,” anakumbuka huku akicheka.

Hii leo, Mwendwa ana zaidi ya kuku 150,000 na lengo lake ni kuwahi milioni moja. “Licha ya shabaha hiyo kuonekana kuwa mbali, ninaamini itawezekana,” anaiambia ‘Akilimali Dijitali’. Kulingana naye, anapanga kufikisha idadi ya kuku 400,000 kufikia Desemba mwaka huu.

Endapo katika miaka ijayo atagonga ndipo, kufikisha idadi ya zaidi ya kuku milioni moja, ataingia kwenye rekodi ya kumbukumbu za Guiness? Guiness World Record, kama inavyofahamika kwa Kiingereza, hata hivyo, haijawahi kuangazia mkulima au mfugaji mwenye idadi ya juu ya kuku.

Nick Mwendwa akikagua mayai kwenye kiangulio. Picha|Sammy Waweru

Kuku mkubwa anayeishi na yai kubwa, ndio pekee imeangaziwa na Guiness World Record. Mwendwa, anasema angetamana sana kuingia kwenye kumbukumbu hiyo ya dunia haswa kwa kufuga idadi ya juu ya kuku halisi wa kienyeji. “Kenya na Afrika kwa jumla, sidhani kunaye (mfugaji) aliyefikisha idadi ya kuku 150,000 ninaofuga kwa sasa,” anahoji.

Rais huyu wa zamani wa FKF alianza ufugaji baada ya kugundua pengo kubwa katika soko la kuku na mayai ya kienyeji. Mwendwa anasema alikuwa akipenda kula kuku wa kienyeji, lakini mara nyingi hakuwa akiwapata kwenye maduka ya kijumla.

Utafiti wake ulionyesha kuwa maduka hayo, maarufu kama supamaketi, yanahitaji kuku halisi wa kienyeji kwa wingi lakini wakulima wengi hawana uwezo wa usambazaji wa kudumu.