Mwanamume kulipa mpenziwe wa zamani Sh2.5m baada picha za siri kusambaa mitandaoni
MAHAKAMA Kuu imeamuru mwanamume mmoja kumlipa Sh2.5 milioni mwanamke aliyeolewa baada ya picha zake za uchi kusambaa mtandaoni, ikisema mtu anayemiliki picha za siri za mwingine ana wajibu wa kuzilinda.
Mahakama ilisema kutozuia picha hizo kusambazwa bila idhini kunaweza kumfanya mhusika kuwajibika, hata kama mwathiriwa hawezi kuonyesha moja kwa moja akaunti iliyozichapisha.
Mwanamume huyo, GH, alipatikana na hatia ya kuchangia kusambaa kwa picha za DN, mpenzi wake wa zamani, kwenye mitandao ya kijamii ikiwemo WhatsApp na Facebook miaka mitatu iliyopita.
Ingawa DN hakuweza kuonyesha kuwa GH ndiye aliyepakia picha hizo, alithibitisha kuwa alikuwa na picha hizo zilizopigwa wakati wa uhusiano wao.
Mahakama ilisema GH alichangia kusambaa kwa picha hizo moja kwa moja, kwa njia isiyo ya moja kwa moja au kwa kutokuwa mwangalifu, na hivyo kukiuka haki za faragha na utu za DN.
DN, ambaye ana watoto wawili, alisema picha hizo zilitumwa kwa marafiki, jamaa na mumewe na kumfanya adharauliwe.
Alisema alipokea simu na jumbe zenye picha hizo na kulazimika kufunga akaunti zake za Facebook na WhatsApp.
Pia alisema alihitaji matibabu na ushauri nasaha baada ya kupata msongo mkubwa wa mawazo.
Kwa mujibu wa DN, picha hizo zilipomfikia mumewe, ndoa yao ilivurugika na akalazimika kurudi kwa wazazi wake pamoja na watoto.
GH alikanusha kusambaza picha hizo. Alisema alifahamu kuwa zilikuwa zikisambazwa baada ya mama yake kumjulisha Machi 23, 2023.
Pia aliambia mahakama kuwa alikuwa amelazwa hospitalini kuanzia Machi 15 hadi 17 kutokana na ugonjwa na hivyo hangeweza kusambaza picha hizo.
Hata hivyo, mahakama ilisema kulazwa hospitalini hakumaanishi kwamba hangeweza kutumia simu yake.
Mahakama pia ilikubali picha za skrini za mitandao ya kijamii licha ya kutowasilishwa kwa cheti kinachohitajika kwa ushahidi wa kielektroniki.
Ilisema ushahidi wa mashahidi, mazingira ya kesi na taarifa nyingine zilithibitisha uhalisi wa picha hizo.
Picha hizo zilionekana kusambazwa kupitia ukurasa uliokuwa na jina “Leaked Videos in Kenya”, lakini hakukuwa na ushahidi wa moja kwa moja uliomtaja GH kama chanzo.
Hata hivyo, mahakama ilisema GH hakutoa maelezo ya kuaminika kuhusu namna picha alizokuwa nazo zilifika kwa umma.
Jaji alisema kumiliki picha za siri kunampa mtu “wajibu mkubwa wa kuhakikisha hazisambazwi bila idhini”.
Mahakama pia ilimzuia GH kuchapisha au kusambaza picha hizo kwa njia yoyote.