Gachagua ataka FBI ichunguze ajali ya ndege iliyomwangamiza Ng’eno
ALIYEKUWA Naibu Rais, Rigathi Gachagua ametaka maafisa kutoka Scotland Yard ya Uingereza na Shirika la Upelelezi la Amerika (FBI) waalikwe nchini kuchunguza ajali ya helikopta iliyomuua aliyekuwa Mbunge wa Emurua Dikirr Johana Ng’eno na watu wengine watano.
Bw Gachagua alisema Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Kenya (KCAA) haziwezi kufanya uchunguzi huru kutokana na maswali mengi ambayo yameibuliwa kuhusu ajali hiyo.
Alisema hayo Ijumaa alipomtembelea mama wa marehemu Ng’eno, Bi Mary Temas, katika kijiji cha Mogondo, Kaunti ya Narok.
“Hatuna imani na polisi wa Kenya na idara nyingine katika suala hili,” alisema Bw Gachagua, akimtaka Rais William Ruto kuwaalika wachunguzi kutoka Uingereza na Amerika.
Ajali hiyo ilitokea Februari 28 katika kijiji cha Chepkiep, eneo bunge la Mosop, Kaunti ya Nandi. Iliwaua Bw Ng’eno, rubani George Were, mpiga picha Nick Kosgei, afisa wa Huduma ya Misitu Kenya (KFS) Amos Kipngetich Rotich, mwalimu Carlos Robert Kibet Keter na afisa wa itifaki katika Serikali ya Kaunti ya Narok Wycliff Kiprotich Rono.
Bw Gachagua alisema familia ya marehemu na Wakenya wana haki ya kufahamishwa ukweli kuhusu kilichosababisha ajali hiyo ili kuondoa shaka iliyopo.
Alidai helikopta hiyo ilisafiri kutoka Endebess, Trans Nzoia, hadi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Eldoret kwa ajili ya kujaza mafuta, lakini ikazuiliwa kwa muda kabla ya kuachiliwa baada ya maafisa wakuu wa serikali kupiga simu.
Kiongozi huyo wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) pia alihoji ubora wa mafuta yaliyotumika na kudai baadhi ya maafisa wa uwanja huo walifutwa kazi katika jaribio la kuficha ukweli.
Alisema maswali kadhaa yameibuliwa tangu ajali hiyo, lakini idara husika za serikali hazijatoa majibu.
Scotland Yard iliwahi kushiriki katika uchunguzi wa mauaji ya raia wa Uingereza Julie Ward katika Hifadhi ya Wanyama ya Maasai Mara mwaka 1988, pamoja na mauaji ya aliyekuwa Waziri wa Masuala ya Kigeni Robert Ouko mwaka 1990.
Familia ya Ng’eno pia ilisema haijawahi kufahamishwa kuhusu maendeleo ya uchunguzi.
Bi Temas alisema serikali haijawahi kuwatembelea tangu mwanawe azikwe na familia imekuwa ikipata taarifa kuhusu uchunguzi huo kutoka kwa watu wengine na mitandao ya kijamii.
“Hakuna mtu aliyekuja hapa kutufahamisha kuhusu hatua iliyofikiwa katika uchunguzi wa kifo cha mwanangu Johana. Watu wa serikali hawajarudi tangu mazishi yake na tuko gizani kabisa,” alisema.
Serikali iliahidi kutoa matokeo ya uchunguzi huo haraka iwezekanavyo, lakini hadi sasa hakuna ripoti iliyotolewa. Hali hiyo imezidisha uvumi kuwa huenda helikopta hiyo ilivurugwa.
Bw Gachagua alizuru familia hiyo miezi mitano baada ya mazishi ya marehemu. Hakuweza kuhudhuria mazishi yaliyofanyika Machi 6 kutokana na mvutano uliokuwapo wakati huo.
Aliwasili Mogondo Ijumaa asubuhi akiandamana na Seneta wa Nyandarua John Methu na mgombea wa DCP katika uchaguzi mdogo wa Mei 14, David Kibet Rotich.
Mbunge wa Emurua Dikirr David Keter na Naibu Gavana wa Narok Tamalinye Koech walikuwa wamemuonya Bw Gachagua kujiepusha na eneo hilo.