Gachagua asema hatafika mbele ya Tume ya NCIC kama alivyoamrishwa
ALIYEKUWA Naibu Rais, Rigathi Gachagua amesema hatafika mbele ya Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) Agosti 27 kama alivyoamrishwa.
NCIC ilimtaka kiongozi huyo wa DCP kufika saa nane alasiri kujibu madai ya kutoa matamshi yanayoweza kuchochea chuki za kikabila katika maeneo ya Vihiga, Kisii na Meru.
Tume ilionya kuwa kutofika kunaweza kusababisha hati ya kukamatwa kutolewa.
Hata hivyo, mawakili wa Gachagua wameiambia NCIC kuwa mteja wao atakuwa nje ya nchi kati ya Agosti 26 na Oktoba 20 kwa safari iliyopangwa kabla ya kuitwa.
Mawakili hao pia wamelalamikia kutowasilishwa kwa ushahidi kamili, wakitaka rekodi halisi za video na sauti pamoja na tafsiri rasmi za baadhi ya matamshi yaliyotolewa kwa Sheng na Gikuyu.
Wanadai matamshi hayo yamechukuliwa nje ya muktadha na hayakuwa na nia ya kuchochea chuki za kikabila.
NCIC bado haijajibu barua hiyo.
Wafuasi wa Bw Gachagua wamekosoa wito huo wakisema tume inatumiwa kisiasa dhidi ya upinzani.