Habari za Kitaifa

Mashirika ya usalama yalipewa Sh44.6 bilioni Julai, ongezeko kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa

Na PETER MBURU August 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WIZARA ya Fedha ilitengea mashirika ya usalama jumla ya Sh44.6 bilioni mwezi Julai, hatua inayodhihirisha ufadhili mkubwa wa sekta hiyo katika mwaka wa mwisho wa serikali kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Kati ya fedha hizo, Wizara ya Ulinzi ilipokea Sh19.4 bilioni, huku Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) na Idara ya Usalama wa Ndani kila moja ikipokea Sh9.9 bilioni.

Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi (NIS) ilitengewa Sh5.4 bilioni.

Fedha zilizotolewa mwezi Julai ziliongezeka kwa asilimia 53 ikilinganishwa na Sh29.1 bilioni zilizotolewa kwa sekta hiyo mwezi Julai mwaka jana, ongezeko kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa katika mwaka unaotangulia uchaguzi mkuu.

Baadhi ya maafisa wa serikali wanahusisha ongezeko hilo na mipango ya kuboresha miundomsingi ya polisi, kuimarisha uwezo wa idara za usalama na kusaidia vitengo vipya vya kiutawala.

Wengine wanachukulia hatua hiyo kama sehemu ya maandalizi ya uchaguzi ujao.

Katibu wa Wizara ya Usalama wa Ndani, Dkt Raymond Omollo, alisema fedha hizo zinalenga kuendeleza mageuzi na kuboresha huduma ya polisi.

“Serikali inaendelea na mpango wa kisasa wa mageuzi ya polisi unaojumuisha uwekezaji katika usafiri, vifaa, miundomsingi, teknolojia na uwezo wa kiutendaji,” alisema.

Kati ya Sh44.6 bilioni zilizotolewa mwezi Julai, Sh39.7 bilioni ni za kugharamia matumizi ya kawaida kama mishahara na gharama za uendeshaji, huku Sh4.9 bilioni zikitengwa kwa miradi ya maendeleo.

Kwa jumla, bajeti ya sekta ya usalama katika mwaka wa kifedha unaoishia Juni 2027 imeongezeka kwa asilimia 26 hadi kufikia Sh510.8 bilioni.

Ongezeko hilo la Sh106 bilioni ni kubwa zaidi ikilinganishwa na wakati wa maandalizi ya uchaguzi wa 2017 na 2022.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Matumizi ya Bunge la Kitaifa Samuel Atandi, alisema sekta ya usalama imekuwa ikihitaji fedha zaidi kwa muda mrefu.

“Hatujawahi kufadhili vya kutosha sekta ya usalama. Tunatarajia kwamba rasilimali zaidi zitakapopatikana, tutapendekeza ongezeko zaidi hasa kwa kuwa tunakaribia mwaka muhimu wa uchaguzi,” alisema.