Habari za Kitaifa

Wakulima wanne wakamatwa uchunguzi kuhusu vifo vya ndovu Amboseli ukiendelea

Na STANLEY NGOTHO August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

OPERESHENI kali ya siku tatu iliyohusisha taasisi mbalimbali katika hifadhi ya wanyamapori ya Amboseli imewawezesha maafisa kuwakamata wakulima wanne.

Wakulima hao wanaojumuisha wanaume watatu na mwanamke mmoja wanashukiwa kuhusika na vifo vya ndovu vilivyosababishwa na sumu katika Kaunti ya Kajiado.

Kukamatwa kwao kunajiri huku idadi ya ndovu waliofariki ikiongezeka kati ya mwezi Juni 24 na Julai 26 ikifikia idadi ya tembo 18.

Maafisa wa huduma ya wanyamapori nchini KWS, pia wamekamata aina mbalimbali za kemikali hatari zinazokisiwa kuwa za sumu, zinazoshukiwa kuingizwa nchini kwa njia ya magendo kutoka nchi jirani. Hatua hiyo imeongeza kasi ya uchunguzi wa chanzo cha vifo hivyo vya kutatanisha. Operesheni hiyo iliyokamilika Ijumaa ilitekelezwa kwa ushirikiano wa pamoja na walinzi wa (KWS), maafisa wa idara ya upepelezi wa jina (DCI) na maafisa wa huduma ya kitaifa ya ujasusi.

Aidha Uchunguzi huo umejumuisha shughuli za utafiti wa maeneo, uchanganuzi wa kina wa maabara pamoja na uchukuaji wa sampuli za mazingira, kwa lengo la kubaini chanzo cha vifo hivyo na kuwafichua waliohusika na mauaji hayo. Kwa mujibu wa takwimu za KWS, Kati ya tembo 16, 10 kati yao walionyesha dalili zinazowiana, zikiwemo kupooza kwa sehemu ya mwili kulikopelekea tembo hao kushindwa kusimama kabla ya kufariki ndani ya siku moja hadi mbili.

Kulingana na ripoti ya awali ya KWS, mizoga mingine ilikuwa imeoza sana au kuliwa na wanyama wengine, hivyo kufanya iwe vigumu kubaini chanzo cha vifo. Vifo hivyo viliathiri zaidi tembo majike waliokomaa pamoja na ndama wao, huku dume mmoja pekee akiwa miongoni mwa waliofariki. Pembe za tembo hao ziliripotiwa kuwa salama wakati wa vifo vyao na baadaye kuondolewa na kuhifadhiwa katika chumba maalum mbugani humo.

Tembo wengine wawili waliokuwa wakipokea matibabu walifariki wiki iliyopita, huku tembo mwingine akiwa katika hali mbaya na akiendelea kutibiwa na madaktari maalum waliobobea kwa masuala ya wanyamapori. Alipothibitisha tukio hilo waziri wa utalii na wanyamapori Rebecca Miano, alitoa taarifa rasmi kwa umma siku ya jumamosi, ambapo alisema matokeo ya awali ya maabara yanaashiria uwezekano wa kuwepo kwa sumu.

Dalili za awali zinaonyesha huenda tembo hao walikufa kutokana na sumu aina ya cyanide, baada ya kula nyanya zilizokuwa zimenyunyiziwa dawa za kuulia wadudu kutoka katika mashamba yaliyopakana na mbuga ya wanyamapori.