Ruto, Gachagua wang’ang’ania kura za Maasai huku Ole Lenku naye akikosana na ODM
VITA vya kisiasa vya kusaka kura za jamii ya Maa vinazidi kupamba moto kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027, huku Rais William Ruto na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua wakiongeza juhudi za kutafuta uungwaji mkono katika jamii ya wafugaji.
Maa ina ushawishi mkubwa katika kaunti za Kajiado, Narok na Samburu, na pia ina idadi kubwa ya wakazi katika baadhi ya maeneo ya Laikipia.
Takwimu za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) zinaonyesha kuwa kaunti hizo tatu zinaweza kuwa na zaidi ya wapigakura milioni 1.4 waliosajiliwa kufikia uchaguzi wa 2027.
Kwa miaka mingi, siasa za Maa zilidhibitiwa pakubwa na mwanasiasa mkongwe William Ole Ntimama, aliyefariki Septemba 1, 2016.
Baada ya kifo chake, eneo hilo lilibaki likimuunga mkono aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, ambaye alifariki Oktoba mwaka jana na kuacha pengo la kisiasa ambalo viongozi mbalimbali sasa wanajaribu kujaza.
Hakuna mwanasiasa kutoka jamii hiyo ambaye ameweza kujaza nafasi iliyowahi kushikiliwa na Bw Odinga na Bw Ntimama.
Juhudi za Seneta wa Narok Ledama Ole Kina kujijenga kama kinara wa Maa pia zinaonekana kudidimia, huku ushawishi wa familia ya Ntutu, inayojumuisha Gavana wa Narok Patrick Ole Ntutu na Mbunge wa Narok Kusini Kitilai Ole Ntutu, ukiendelea kupungua.
Rais Ruto alitembelea Narok Jumanne na kuwataka wakazi kumpima kwa rekodi yake ya maendeleo.
“Wakenya wanataka maendeleo wala si maneno matupu. Narok ni kaunti yenye utajiri wa kilimo na hakuna sababu kwa nini msipate barabara nzuri,” akasema Rais.
Alizindua ujenzi wa barabara ya Enengetia-Olkurto-Olposimoru yenye urefu wa kilomita 59 na kutaja miradi mingine ya barabara inayoendelea katika kaunti hiyo.
Pia alisema Sh2.8 bilioni zitatumika kuunganisha nyumba 15,000 zaidi na umeme. Alisema nyumba 14,000 zimeunganishwa na umeme katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Kwa upande wake, Bw Gachagua ameendelea kuvutia jamii ya Maa kwa usaidizi wa Seneta wa Kajiado Seki Lenku na Mbunge wa Kajiado Kusini Samuel Parashina.
Alitembelea Narok Agosti 21, ambako alizuru Emurua Dikirr na kaburi la aliyekuwa mbunge Johana Ng’eno.
Mbunge wa Kajiado ya Kati Memusi Kanchory alisema viongozi wanaounga mkono Serikali Jumuishi wanaunga mkono azma ya Rais Ruto ya kuchaguliwa tena 2027.
“Hapa tuko kwa mihula miwili na tunafanya kazi katika Serikali Jumuishi, lakini kuna viongozi ambao wameazimia kutugawanya kwa sababu hawafurahishwi na ushirikiano wetu,” akasema Bw Kanchory.
Gavana wa Kajiado Joseph Ole Lenku, hata hivyo, amekosana na ODM na ametishia kutafuta chama kingine atakachotumia kuwania useneta wa Kajiado.
“Tulipata ODM ikiwa dhaifu na kwa sababu tulimheshimu aliyekuwa Waziri Mkuu marehemu Raila Odinga, tuliimarisha chama hicho Kajiado. Kama vile madiwani wa UDA walivyojiunga na DCP, sisi pia tutaondoka na kujiunga na Linda Mwananchi,” akasema Bw Lenku.
“ODM itafunga shughuli zake katika Kaunti ya Kajiado. Sisi ndio tulileta ODM hapa na kuifanya iheshimike,” akaongeza.
Kwa upande wake, Bw Gachagua amejitaja kama mtetezi wa maslahi ya Maa, hasa kuhusu suala la ardhi.
“Raila Odinga amekuwa akiwatetea tangu zamani. Mungu amemchukua. Nataka mnifanye kuwa mtetezi wenu. Nitatetea na kusimamia maslahi yenu bila woga, hasa kuhusu suala la ardhi,” akasema wakati wa ziara yake Kajiado Februari mwaka huu.
Katika uchaguzi wa 2022, Raila alishinda Ruto katika kaunti zote tatu. Kajiado alipata kura 158,526 dhidi ya 148,439 za Ruto, Narok alipata 102,279 dhidi ya 92,894, huku Samburu akipata 41,737 dhidi ya 28,319.