Siasa

Gachagua sasa ‘ammaliza’ Uhuru Mlimani na Nairobi

Na MOSES NYAMORI, DANIEL OGETTA August 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha DCP kinachoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kinazidi kujitokeza kama tishio kubwa kwa Jubilee, chama cha aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta, huku kikivamia ngome zake za kisiasa za Mlima Kenya na Nairobi.

Huku Uchaguzi Mkuu wa 2027 ukikaribia, Jubilee imepata pigo jingine, viongozi wake kadhaa waliochaguliwa wakitangaza kuhamia DCP.

Mbunge wa Kamukunji Yusuf Hassan ndiye wa hivi punde kuondoka Jubilee, hatua inayoonyesha kuwa ushindani kati ya vyama hivyo haupo katika eneo la Mlima Kenya pekee.

Nairobi, wabunge wote watatu waliochaguliwa kwa tiketi ya Jubilee wametangaza kuwa watatetea viti vyao kwa tiketi ya DCP.

Hao ni Bw Hassan, Mark Mwenje wa Embakasi Magharibi na Amos Mwago wa Starehe.

Mlima Kenya, Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) Kanini Kega, aliyedhaminiwa na Jubilee, pia amehamia DCP.

Viongozi wengine wa Jubilee, wakiwemo wabunge walioteuliwa Sabina Chege, Aden Keynan (Eldas), Samuel Arama (Nakuru Mjini Magharibi), John Waluke (Sirisia) na Racheal Nyamai (Kitui Kusini), wameegemea Serikali Jumuishi.

Kuhama huku kunaweza kudhoofisha uwezo wa Bw Kenyatta kujadiliana kisiasa kuelekea 2027 na kumfanya Bw Gachagua kuwa mhusika mkubwa katika siasa za upinzani.

Akizungumzia hatima ya Jubilee, Bw Kega alisema wazi kuwa chama hicho kimekufa kisiasa Mlima Kenya na Nairobi.

“Hakuna Jubilee Mlima Kenya na Nairobi. Tatizo linaloikabili Jubilee ni ukosefu wa uongozi. Tulipojaribu kufanya mabadiliko, yalipingwa, na sasa mnaona kinachotokea. Kila mtu anaondoka,” akasema Bw Kega.

Hata hivyo, Naibu Kiongozi wa Jubilee Jeremiah Kioni alipuuza kuhama kwa viongozi hao, akisema wengi wao hawakuwa waaminifu kwa chama hicho na walikitumia tu kupata nyadhifa serikalini.

“Si hasara mpya kwetu kwa sababu hawajawahi kujitambulisha na Jubilee. Kwa kweli, ni fursa kwetu kutafuta vijana ambao wamejitolea kuwa nguzo wa chama,” akasema Bw Kioni.

Alidai kuwa DCP inaonekana kujishughulisha zaidi na kupambana na Jubilee kuliko UDA.

Bw Gachagua, hata hivyo, alitangaza Jumanne kuwa DCP imechukua usukani wa siasa za Nairobi baada ya Bw Hassan kujiunga na chama hicho.

“Ninataka kutangaza leo kwamba DCP imechukua Nairobi,” akasema kiongozi huyo wa DCP.

Naibu kiongozi wa DCP Cleophas Malala alisema kuhama kwa Bw Hassan ni ushahidi kuwa chama hicho kinageuka kuwa na sura ya kitaifa, huku Katibu Mkuu John Methu akiahidi uteuzi wa haki kwa wagombeaji.

“Nimejiunga na DCP kwa sababu ni chama kinachotaka mabadiliko halisi,” akasema Bw Hassan.

Kwa kuhama huku, vita vya kisiasa kati ya DCP na Jubilee vinaonekana kuingia katika hatua mpya, huku Nairobi na Mlima Kenya zikitarajiwa kuwa maeneo muhimu ya mapambano kuelekea 2027.