Makala

Mbunge aandaa mbio za baiskeli kuboresha afya, kuhubiri amani

Na KALUME KAZUNGU August 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ZAIDI ya watu 500 walijitokeza eneo la Baharini, tarafa ya Mpeketoni, Lamu Magharibi kushuhudia mbio za baiskeli.

Mashindano hayo yaliyodhaminiwa na ofisi ya Mbunge wa Kike wa kaunti ya Lamu, Bi Muthoni Monica Marubu yalidhamiria kuhubiri amani, umoja na utangamano msimu huu ambapo Uchaguzi Mkuu wa 2027 unaendelea kukaribia.

Wakati wa mbio hizo, mashabiki waliojitokeza pamoja na walioshirikishwa mchezoni kuelimishwa kuhusiana na umuhimu wa kuendelea kujisajili kama wapigakura na kushiriki kikamilifu uchaguzi mkuu ujao.

Isitoshe, mbio hizo zilinuiwa kuwasaidia wazee, akina mama, vijana na watoto kujenga afya ya miili yao wanapoendesha baiskeli hizo.

Kina mama wakisubiri zamu yao kushiriki mashindano ya kuendesha baiskeli yaliyoandaliwa na Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Lamu Muthoni Monica Marubu. Picha|Kalume Kazungu

Mbio hizo ziligawanywa makundi tofautitofauti, ikiwemo wazee na akina mama wa umri wa kati ya miaka 50 hadi 70, vijana waliokomaa na wale wa kizazi cha Gen Z na watoto.

Walioibuka washindi katika kila kitengo cha mashindano hayo ya mbio za baiskeli walitunukiwa baiskeli mpya.

Mbali na kijiji cha Baharini, mbio hizo pia zimewahi kuandaliwa katika mji wa Mpeketoni, Hindi, Safirisi na viunga vyake.

Sehemu zingine zinazolengwa kuwashirikisha wananchi katika mbio sawia ni Witu, kisiwa cha Lamu, kilecha Manda na maeneo ya Lamu Mashariki.

“Nimefurahi kuona wananchi, ikiwemo wazee wakongwe, akina mama, vijana na watoto, wote wakitangamana na kufurahia mbio za baiskeli hapa Baharini. Wameonyesha weledi wao katika kuendesha baiskeli, kuijenga afya ya miili yao, kuhubiri amani na uwiano. Ningewasihi wakazi kote Lamuna nchini wajikaze kujisajili kama wapiga kura wakati uchaguzi mkuu ukikaribia,” akasema Bi Marubu.

Umati uliohudhuria mashindano ya baiskeli yaliyoandaliwa na Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Lamu Muthoni Monica Marubu. Picha|Kalume Kazungu

Aliongeza, “Hii pia ni sehemu mojawapo ya mimi kama kiongozi kujishirikisha na wananchi mashinani ili kuwapa ajenda zangu za uongozi na kupokea ushauri au maoni kutoka kwao kuhusiana na ni lipi nafaa kuwafanyia.”

Issakia Yunus, kiongozi wa vijana Lamu, alimpongeza Bi Marubu kwa kuibuka na mfumo huo alioutaja kujenga umoja wa wananchi.

“Tumejionea maafisa wa utawala serikalini,ikiwemo machifu wetu na walinda usalama wakijumuika na wananchi kwenye mbio za baiskeli. Huko ni kumaanisha mashindano kama haya hayaleti umoja Lamu pekee bali pia kitaifa,” akasema Bw Yunus.