Ruto: Serikali lazima ipewe nafasi kutekeleza ahadi zake
RAIS William Ruto ameibua mjadala kuhusu nafasi ya Serikali iliyochaguliwa kutekeleza manifesto yake bila kuingiliwa na mahakama.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya 16 ya Katiba ya 2010 jijini Nairobi, Rais Ruto aliuliza ni kiasi gani cha nafasi Katiba inapaswa kupatia serikali iliyochaguliwa kutekeleza mpango ambao uliifanya ishinde uchaguzi.
“Serikali iliyochaguliwa inapaswa kuwa na nafasi ya kikatiba kiasi gani kutekeleza mpango ambao ilichaguliwa kuutekeleza?” Rais aliuliza.
Alisema changamoto hujitokeza wakati mipango ya Serikali inapopingwa mahakamani, akitaka kuwe na tofauti kati ya mahakama kuchunguza uhalali wa hatua za Serikali na kufanya maamuzi ya sera ambayo ni jukumu la taasisi zilizochaguliwa.
Hata hivyo, Rais alisema uhuru wa Mahakama haupaswi kuhojiwa.
“Mahakama lazima ibaki huru kutafsiri Katiba, kulinda haki na kubatilisha hatua zisizo halali,” alisema.
Aliongeza kuwa Serikali inapokiuka sheria, inapaswa kuheshimu maagizo ya mahakama na kurekebisha mwenendo wake.
Lakini alisema sera halali zinazotekelezwa ndani ya mamlaka ya taasisi zilizochaguliwa zinapaswa kuheshimiwa.
“Kura hutoa mwelekeo. Katiba huweka mipaka. Taasisi za umma huhakikisha mambo hayo mawili yanaheshimiwa,” alisema.
Kauli hiyo inajiri huku baadhi ya miradi mikuu ya Kenya Kwanza ikikumbwa na changamoto za kisheria, hasa kuhusu haki za wananchi, matumizi ya fedha za umma na mipaka ya mamlaka ya Serikali.
Rais alitaja huduma ya afya kwa wote, nyumba za bei nafuu, utoshelevu wa chakula, elimu na ulinzi wa kijamii kuwa nguzo za ajenda yake ya mabadiliko ya kiuchumi.
Aliuliza iwapo uchunguzi wa mahakama unaweza wakati mwingine kusababisha utekelezaji wa sera halali za Serikali kucheleweshwa.
“Tunawezaje kulinda uchunguzi wa mahakama bila kuzorotesha utekelezaji halali wa Serikali? Tunawezaje kuhakikisha mfumo wa kuangalia na kusawazisha mamlaka unabaki kuwa chombo cha uwajibikaji badala ya kusababisha taasisi kukwama?” aliuliza.
Rais pia alizungumzia maandamano ya Gen Z ya 2024, akisema vijana walikuwa wakitumia haki zao za kikatiba na walitaka kusikilizwa.
Alisema vijana walitumia haki za kuzungumza, kukusanyika, kuandamana na kuwasilisha malalamiko kwa serikali.
“Ujumbe wao ulikuwa wazi: walitaka kusikilizwa. Walitaka uwajibikaji zaidi, serikali bora na nafasi ya maana katika kuamua mustakabali wa taifa lao,” alisema.
Kauli hiyo ni tofauti na ile aliyotoa Juni 25, 2024, alipotaja maandamano hayo kuwa “uhaini”.
Rais pia alikiri madai ya ukiukaji wa haki za binadamu wakati wa maandamano hayo, yakiwemo kukamatwa kiholela, watu kutoweka na matumizi ya nguvu kupita kiasi.
Alisema kila madai ya ukiukaji wa haki yanayoweza kuthibitishwa yanapaswa kuchunguzwa kwa kina na kwa uwazi, na waliohusika wawajibishwe.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa haki ya kuandamana haijumuishi vurugu, uporaji au uharibifu wa mali.
Naibu Rais Kithure Kindiki alisema maadhimisho hayo yalikuwa fursa ya kutafakari hatua ambazo Kenya imepiga katika kudumisha umoja na kuvumiliana.
Kwa upande wake, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka alisema kutoheshimiwa kwa maagizo ya mahakama ni tishio kwa utawala wa sheria.
Alisema pia ukiukaji wa haki za waandamanaji na kutotekelezwa kwa Sura ya Sita kuhusu uongozi na uadilifu kunaweza kudhoofisha Katiba.
Alionya kuwa uchaguzi ukisimamiwa vibaya au matokeo yake kuibwa, suala hilo linaweza kubadilika kutoka tatizo la kisheria na kuwa la kiusalama na kibinadamu.
“Hatupaswi kurudi huko tena,” alisema.