Muhoozi kuwania urais 2031 akisema babake, Rais Museveni, atamuunga mkono
KAMPALA, Uganda:
MKUU wa jeshi la Uganda, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ambaye pia ni mwana wa Rais Yoweri Museveni, ametangaza kuwa atawania urais katika uchaguzi wa mwaka 2031.
Kainerugaba, mwenye umri wa miaka 52, kwa muda mrefu ametajwa kuwa mrithi anayetarajiwa wa baba yake mwenye umri wa miaka 81, ambaye ametawala Uganda kwa miongo minne.
Mkuu huyo wa jeshi pia anafahamika kwa jumbe zake zenye utata kwenye mtandao wa kijamii wa X, zikiwemo tishio la kumkata kichwa kiongozi mkuu wa upinzani, Bobi Wine.
Katika ujumbe mmoja kati ya mfululizo wa machapisho aliyoweka X Jumanne usiku, Kainerugaba alisema alikuwa tayari kuwania wadhifa wa juu zaidi nchini humo.
“Nitawania wadhifa wa juu zaidi nchini mnamo 2031. Na tutashinda kwa neema ya Mwenyezi Mungu,” akasema Kainerugaba.
Aliongeza kuwa kwa kuungwa mkono na baba yake, ambaye huwa anamrejelea kwa heshima kama “Mzee”, ana uhakika wa kupata asilimia 90 ya kura katika uchaguzi huo.
Kainerugaba, ambaye anaongoza kundi la wazalendo wa Uganda (PLU), hapo awali alikuwa ametangaza kuwa angewania urais katika uchaguzi uliofanyika Januari mwaka huu, lakini baadaye akajiondoa na kumuunga mkono baba yake.
Alikuwa na nafasi muhimu katika kampeni za kuhakikisha Museveni anachaguliwa tena Januari, huku akiamuru hatua kali dhidi ya wapinzani na kuzimwa kwa intaneti, kulingana na ripoti zilizozingira uchaguzi huo tata.
Museveni, ambaye anaongoza chama tawala cha National Resistance Movement (NRM), amekuwa madarakani tangu 1986.
Wakosoaji wamekuwa wakiilaumu serikali yake kwa ukiukaji wa haki za binadamu, yakiwemo mateso, utekaji nyara na kuwazuilia watu kiholela, madai ambayo serikali imekanusha.
Bobi Wine alikimbilia Amerika mapema mwaka huu, akisema alihofia maisha yake baada ya kupinga ushindi wa Museveni akidai kulikuwa na visa vya udanganyifu.
Mwanasiasa mwingine mkongwe wa upinzani, Kizza Besigye, amekuwa gerezani tangu 2024 na anakabiliwa na kesi ya uhaini.
Licha ya afya ya Besigye kuendelea kudorora, utawala wa Museveni hauonekani kumakinikia kumwaachilia huru.
Haijulikani iwapo Museveni mwenyewe atawania tena urais 2031 baada ya tangazo lake, huku serikali ikisema uamuzi huo utafanywa na rais pamoja na chama chake kwa wakati mwafaka.
Mnamo 2031, Museveni atakuwa na umri wa miaka 86 na akiwania, atakuwa kati ya viongozi wakongwe zaidi ambao wamewahi kuwania wadhifa wa urais ulimwenguni.