Wafanyakazi wa KPA wahofia kupoteza kazi serikali ikitafuta wawekezaji wa kibinafsi
WAFANYAKAZI wa Mamlaka ya Bandari nchini (KPA) wameingiwa na wasiwasi kuhusu mustakabali wa ajira zao huku serikali ikijiandaa kuwapa wawekezaji binafsi nafasi ya kuendesha baadhi ya shughuli katika bandari za Mombasa na Lamu.
Wasiwasi huo umeibuka baada ya Kamati ya Ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPP) kuidhinisha tafiti za uwezekano wa kuhusisha sekta binafsi katika vituo muhimu vya bandari.
Mkurugenzi Mkuu wa tume ya mipango ya uwekezaji kati ya umma na kampuni za kibinafi (PPP) Kefa Seda alisema Alhamisi kuwa uamuzi huo umefungua njia ya kuanza mchakato wa zabuni mwezi Septemba.
Mali zitakazohusika katika awamu ya kwanza ni Gati 11 hadi 14 za Bandari ya Mombasa, Mombasa Container Terminal 1, Lamu Container Terminal na Eneo Maalum la Kiuchumi la Lamu (SEZ).
“Uidhinishaji huu unahamisha mali hizi muhimu za bandari kutoka hatua ya utafiti hadi hatua ya ununuzi chini ya mfumo wa PPP,” Bw Seda alisema.
Mpango huo ni sehemu ya mabadiliko ya bandari za Mombasa na Lamu kuwa mfumo wa ‘landlord port’, ambapo serikali itaendelea kumiliki mali hizo huku sekta binafsi ikisimamia shughuli za kila siku.
Hata hivyo, wafanyakazi wana hofu kuwa mpango huo unaweza kusababisha kupunguzwa kwa nafasi za ajira au kubadilishwa kwa mikataba yao.
Wasiwasi huo umeongezwa na zabuni ya KPA ya kukodisha vifaa na huduma za uendeshaji, inayotaja kuajiri takriban wafanyakazi 4,700 wenye ujuzi maalum.
“Kufikia sasa hatujui hatima yetu baada ya zabuni hii kuchapishwa. Wasiwasi wetu mkubwa ni aina ya wafanyakazi wanaohitajika bandarini,” alisema mfanyakazi mmoja wa KPA.
Nyaraka za mpango huo zinawapa wafanyakazi chaguo la kubaki KPA, kuhamishiwa taasisi nyingine za serikali au kutumwa kwa kampuni binafsi kwa hiari.
Mkurugenzi Mkuu wa KPA, Kapteni William Ruto, amekanusha madai kwamba bandari inauzwa, akisema serikali itaendelea kuwa mmiliki wa miundombinu.
Alisema sekta binafsi italeta mtaji na utaalamu ili kuboresha ufanisi wa bandari.
Bandari ya Mombasa ilihudumia tani milioni 45.45 za mizigo mwaka jana, kutoka tani milioni 40.99 mwaka 2024, huku trafiki ya makontena ikizidi TEU milioni 2.11.
Kwa sasa, wafanyakazi wanataka serikali iwape hakikisho kuhusu ajira zao kabla ya mchakato wa zabuni kuanza mwezi ujao.