Wafanyabiashara waandamana wakilalamikia ushuru wa juu
BIASHARA ziliathirika jijini Nairobi jana huku wafanyabiashara wadogo wakimiminika barabarani kupinga kile walichokitaja kuwa ongezeko la ushuru na ukadiriaji mpya wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje uliowekwa na Mamlaka ya Mapato Kenya (KRA).
Waandamanaji walikusanyika katika eneo la Archives kabla ya kuandamana kuelekea makao makuu ya KRA katika jengo la Times Tower katikati mwa jiji.
Wafanyabiashara hao walisema mabadiliko ya kiwango kinachotumiwa kukadiria thamani ya bidhaa za uagizaji yameongeza gharama za biashara na kupunguza faida zao.
Kwa mujibu wao, KRA imepandisha kiwango cha ukadiriaji kutoka 2.5m hadi 3.2m, hatua wanayodai imeongeza kwa kiasi kikubwa kodi inayolipwa kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje, hususan kutoka China.
Walisema mabadiliko hayo yamesababisha ongezeko la takriban asilimia 28, huku thamani ya bidhaa kwa madhumuni ya kodi ikiongezeka kutoka Sh2.5 milioni hadi Sh3.2 milioni.