Habari

Wabunge wa ‘Broabased’ wakosolewa kwa uzembe kamatini

Na EDWIN MUTAI August 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WABUNGE wanaounga mkono serikali ambao wanaongoza kamati muhimu za Bunge wamekosolewa kwa kushindwa kuwawajibisha mawaziri kuhusu masuala yanayowahusu wananchi.
Ripoti iliyowasilishwa na Naibu Kiongozi wa Wengi katika Bunge, Owen Baiya, ilifichua kuwa kamati 19 za Bunge zilikuwa zimeshindwa kutoa majibu kwa maswali yaliyoulizwa na wabunge kwa niaba ya wananchi kufikia wakati Bunge lilipoenda likizo ya mwezi mmoja Alhamisi.
Kamati ya Utawala na Usalama wa Ndani iliongoza kwa kuwa na maombi 26 ambayo hayakuwa yamejibiwa. Kamati hiyo inaongozwa na Mbunge wa Narok West, Gabriel Tongoyo.
Kamati ya Uchukuzi na Miundombinu, inayoongozwa na Mbunge wa Ndia George Kariuki, ilikuwa ya pili kwa kuwa na maswali 21 ambayo hayajajibiwa kuhusu kuimarishwa kwa miundombinu.
Kamati ya Elimu inayoongozwa na Mbunge wa Tinderet Julius Melly ilikuwa na maswali 18 ambayo hayajajibiwa kuhusu sekta ya elimu.
 Bw Tongoyo, Bw Kariuki na Bw Melly walichaguliwa kwa tiketi ya UDA, chama tawala katika serikali ya Kenya Kwanza.
Ripoti hiyo iliandaliwa kwa maagizo ya Spika wa Bunge Moses Wetang’ula baada ya wabunge kutaka kujua hatua zilizochukuliwa kuhusu maombi yao ya taarifa.
 “Wabunge wanahitaji kujua jinsi maombi yao ya taarifa yalivyoshughulikiwa na kamati mbalimbali,” alisema Bw Baiya alipowasilisha ripoti hiyo.
 Bw Baiya aliwataka wenyeviti wa kamati kuhakikisha majibu kutoka kwa mawaziri na mashirika ya serikali yanawasilishwa kwa wakati.
 “Wanafanya hivyo kwa niaba ya wapigakura wao. Hilo linatulazimu sisi kama wenyeviti wa kamati kuhakikisha yanajibiwa kwa ufupi, kwa usahihi na kwa wakati. Hii itahakikisha Bunge halifanyi kazi bure,” akasema.
Kamati za Afya na Fedha na Mipango ya Kitaifa, zinazoongozwa na James Nyikal (Seme) na Kuria Kimani (Molo), kila moja ilikuwa na maombi manane ambayo hayajajibiwa.
Kamati ya Ardhi, inayoongozwa na Joash Nyamoko (Mugirango Kaskazini), ilikuwa na maswali saba, huku Kamati ya Ulinzi, Ujasusi na Uhusiano wa Kimataifa ikiwa na sita.
Kamati za Kilimo na Mifugo, Nishati na Leba kila moja zilikuwa na maswali matano ambayo hayajajibiwa.
Kamati ya Mazingira, Misitu na Madini ilikuwa na manne, huku kamati za Utalii na Wanyamapori na Nyumba, Mipango Miji na Kazi za Umma kila moja ikiwa na matatu.
Kamati nyingine zilizokuwa na maswali ambayo hayajajibiwa ni Mawasiliano, Habari na Ubunifu (mawili), Sheria na Haki (moja), Ulinzi wa Jamii (moja), Biashara, Viwanda na Vyama vya Ushirika (moja) na Bajeti na Matumizi (moja).
Wabunge hupokea posho za vikao vya kamati pamoja na mshahara na marupurupu mengine. Mwenyekiti wa kamati hupokea Sh15,000 kwa kila kikao, hadi kiwango cha juu cha Sh240,000 kwa mwezi.