Wanasema utahitaji kuwa imara kisaikolojia kufaulu katika biashara ya majeneza: Tambua kivipi
WATENGENEZAJI na wauzaji majeneza Pwani wanakiri kuvuna pakubwa na kujijenga kimaisha licha biashara hiyo kuwa na changamoto tele, hasa kimtazamo wa jamii.
Mafundi na wauzaji wa majeneza waliohojiwa na Akili Mali katika kaunti za Kilifi, Mombasa, Kwale, Taita Taveta na Mpeketoni (Lamu) walisisitiza kuwa biashara hiyo ina malipo ya kuridhisha ila inahitaji ustahimilivu mkubwa wa kisaikolojia kutokana na mtazamo uliopo wa jamii na mazingira yenyewe ya kikazi.
George Kirao Nzaro, 26, ambaye ni fundi na muuzaji majeneza mjini Malindi, Kaunti ya Kilifi, amedumu kwenye biashara hiyo kwa karibu miaka minane sasa.
Alijitosa katika kazi hiyo 2018 mwaka mmoja baada ya kuacha masomo yake ya kidato cha kwanza kutokana na ukosefu wa karo.
Alipokea ujuzi kupitia duka moja la mbao lililomwajiri na ambalo pia lilishughulikia masuala ya majeneza mjini Kilifi.
Ni kutokana na ujuzi na ustadi aliopokea uliomfanya kubadilisha makazi yake ya kazi, hivyo kuhama kutoka kijiji chao cha Misufini, viungani mwa mji wa Kilifi na kufungua eneo lake binafsi la Heri Directors lililoko mtaa wa Seabreeze mjini Malindi.
Kwenye duka hilo, Kirao huchonga mbao, kuzipiga msasa, kugonga na kuunda majeneza kabla ya kuyatia nakshi na rangi tayari kwa wateja.
Anasema yeye hakosi angalau Sh90,000 kila mwezi kupitia uundaji na uuzaji wa majeneza na wakati mwingine huunda hadi Sh250,000.
“Kuna nyakati ambapo unajipata umekaa tu ukisubiri hadi wiki mbili au mwezi mzima bila kuuza jeneza lolote. Ni biashara inayohitaji uvumilivu kwani huwezi kuombea mtu afe. Ila kuna msimu utapata biashara ikinawiri kwa kuuza majeneza mengi, hivyo kupata hela ya juu,” anasema Kirao.
Kariuki Kimani, mfanyibiashara na mmiliki wa duka la majeneza na huduma nyingine za mazishi, ikiwemo usafirishaji maiti la Eureka Supreme Services lililoko katikati mwa mji wa Mpeketoni, Kaunti ya Lamu, anaitaja biashara hiyo kuwa muhimu kwa jamii, akiwasihi vijana kutoibagua.
Amedumu kwenye biashara hiyo karibu miaka kumi. Yeye huuza jeneza moja kwa kati ya Sh10,000 hadi Sh50,000, ukadiriaji wa bei kwake ukitegemea ukubwa wa jeneza, muundo, aina, urembo, hadhi au tabaka ambalo mteja atataka.
“Tuko na hadi hadhi au tabaka la VIP kwa wanaotafuta huduma zetu, iwe ni jeneza, usafirishaji marehemu, mahema hadi maziko,” anaeleza.
“Jamii ifahamu kuwa kazi ya majeneza ina kipato. Kipato hicho kisingekuwepo basi duka langu halingedumu miaka yote kumi”
Abdallah Mainge, mfanyibiashara wa majeneza, usafirishaji wa maiti na mazishi anayemiliki duka la Malindi Funeral Services and Coffin Centre lililoko mkabala na Hospitali Kuu ya Kaunti Ndogo ya Malindi, anaisifu biashara hiyo kwa kumsaidia kuyakimu maisha yake na ya familia pia. Alianza kazi hiyo 2017.
“Mwaka 2017 kulikuwa na sintofahamu za kisiasa kidogo nchini, hali iliyopelekea biashara ya utalii kusambaratika. Nikalazimika kugeuza gari langu kuwa la kusafirishia maiti.
Huduma ya kusafirisha maiti kutoka mji wa Malindi hadi Gede au Gongoni ilikuwa kati ya Sh10,000 hadi Sh25,000 kwa wakati huo. Hapo ndipo nikatambua kuwa nyanja hii ya matanga pia ina kipato,” anaeleza.
Baadaye alipanua huduma zake, ambapo mbali na kusafirisha maiti kwa maziko, pia aliafikia kufungua duka lake la Malindi Funeral Services and Coffin Centre ili kuuza jeneza, nguo za kuvalisha maiti, mahema, mapambo ya matangani nakadhalika.
Yeye huuza jeneza moja kati ya Sh15,000 hadi zaidi ya Sh100,000 akishikilia kuwa bei pia inakadiriwa kulingana na matakwa ya mteja mwenyewe.
Kwa mwezi yeye hakosi kati ya Sh100,000 hadi Sh200,000 japo anashikilia kuwa mapato hayo hubadilikabadilika kulingana na misimu.
“Ninapeana huduma mbalimbali. Hapa utapata majeneza ya bei tofauti. Kuna yale ya kawaida hadi ya kifahari yanayouzwa kwa maelfu ya fedha kulingana na uwezo wa mteja,” akasema Bw Mainge.
Anakiri kuwa biashara ya kuuza jeneza ina changamoto tele kwani miongoni mwa mambo magumu zaidi maishani mwake ni kujaribu kujadiliana bei na mteja ambaye tayari amefiliwa akiwa maombolezoni.
“Sisi wenye biashara hizi lazima tuwe na mioyo migumu na pia kuelewa wateja wetu ambao tayari wamepatwa na msiba tunapojadiliana bei. Watu wengi awali waliogopa biashara ya majeneza na kusafirisha maiti wakidhani sisi hushangilia kifo ili tupate pesa. La hasha. Hii ni mojawapo ya mbinu ya kusaidia jamii zetu manake tusipokuwepo itamaanisha kutakuwa na tatizo la watu kuzikwa,” akasema Bw Mainge.
Anaililia serikali ya Kaunti ya Kilifi na ile ya kitaifa kupunguza makato ya kodi wanayolumbikiziwa kila mara bila kujali jinsi biashara zao zinavyohudumu, iwe ni katika hali nzuri au misimu ya chini.
“Awali tulikuwa tukikatwa kodi ya mwaka ya Sh6,000 na kaunti yetu ya Kilifi. Kwa sasa makato yamepandishwa hadi karibu Sh14,000 ambayo ni karibu mara mbili ya makato ya awali. Wafanye jambo. Tunaumia,” akasema Bw Mainge.
Kahindi Mdzomba, mmiliki na muuzaji majeneza eneo la Makadara katika jiji kuu la Mombasa, pia anaitaja biashara ya majeneza kuwa ya kutegemeeka kimapato.
“Biashara hii ya majeneza siyo rahisi vile. Tunakubali kwamba inatatiza kisaikolojia. Waonaje wewe hii hali ya kufanya kazi huku ukizungukwa na ishara za maombolezo na simanzi kila siku? Ni biashara inayohitaji uwe na akili dhabiti na ujasiri. Imetujenga kimaisha,” akasema Bw Mdzomba.
Anasema kila mwezi hakosi angalau Sh60,000 ambayo ni faida hasa baada ya kuwalipa wasaidizi wake anaofanya kazi nao dukani kwake.
Naye Stephen Mwabili, muuzaji majeneza mjini Voi, Taita Taveta, alisema changamoto kuu wanayokumbana nayo kila siku kazini ni kushughulikia wateja walio katika majonzi makubwa, jambo linalohitaji uvumilivu na busara ya hali ya juu.
Kwa upande wake, Solomon Ndegwa, fundi wa majeneza katika duka lililoko mkabala na hospitali ya rufaa ya Msambweni, Kaunti ya Kwale, anasema kazi ni kazi.