Orengo: Mimi ndio nimeiva kuwa rais na nitashindana na Sifuna kwa tiketi 2027
GAVANA wa Siaya James Orengo amemtaka Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na wagombeaji wengine ndani ya Linda Mwananchi kukubali uteuzi wa wazi wanaposaka mwaniaji wao wa urais kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Katika mahojiano na Taifa Leo Jumanne, Bw Orengo alisema hana tatizo kushindana na Bw Sifuna au mgombea mwingine yeyote wa upinzani.
Alisisitiza jambo muhimu ni kuhakikisha vuguvugu hilo linapata mgombea mmoja wa kukabiliana na Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027.
“Hakuna ubaya kwa wagombea mbalimbali kuwa na azma ya urais ndani ya Linda Mwananchi au upinzani. Muhimu ni kuwapa wote fursa ya kupitia mchakato wa uteuzi wa wazi na wa kuaminika, ili hatimaye tupate mgombea mmoja wa kukabiliana na Ruto. Huo ndio msingi wa umoja wa upinzani,” akasema Bw Orengo.
Gavana huyo mkongwe alisisitiza kuwa uteuzi haupaswi kuamuliwa katika vikao vya siri, akitaja uchaguzi wa urais wa ODM wa 2007 ambapo Raila Odinga, William Ruto, Musalia Mudavadi, Najib Balala na Joe Nyaga walishindana kabla ya chama kumpata mgombea wake.
Alitaja pia uchaguzi wa 2002, ambapo vyama vya upinzani vilifanya mashauriano kabla ya Bw Odinga, aliyekuwa akiongoza LDP, kumuunga mkono Mwai Kibaki kupitia kauli ya “Kibaki Tosha”.
Bw Orengo alisema mifano hiyo inaonyesha kuwa umoja wa upinzani hauhitaji kuondoa mapema azma za wagombea mbalimbali wenye nia ya kusaka urais.
Ingawa hivyo, msimamo wake umemweka pabaya na washirika wa Bw Sifuna, ambao wamekuwa wakisema wafuasi wa Linda Mwananchi tayari wameamua kumuunga mkono seneta huyo wa Nairobi.
Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya ni miongoni mwa viongozi wa Magharibi waliomuunga mkono Bw Sifuna na kusema wananchi wamekuwa wakisema “Sisi Ndio Sifuna” katika mikutano ya vuguvugu hilo.
Mbunge wa Kabuchai Majimbo Kalasinga alisema hakuna haja ya kuchanganya wafuasi kwa kujitokeza kwa wagombea wengine.
“Hatupaswi kuchanganyikiwa. Wakenya wamejitokeza katika kila mkutano wa Linda Mwananchi na kusema wanamtaka Edwin Sifuna kuwa mgombea wa urais,” akasema Bw Kalasinga.
Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, hata hivyo, alisema vuguvugu hilo linamheshimu Bw Orengo kutokana na uzoefu wake wa kisiasa na mchango wake katika masuala ya mageuzi.
“Vuguvugu linamheshimu sana Gavana Orengo kutokana na hadhi na uzoefu wake mkubwa katika masuala ya mageuzi,” akasema Bw Osotsi, akiongeza kuwa kutakuwa na utaratibu wa kutatua suala hilo wakati ufaao.
Mwanasiasa wa Jubilee Pauline Njoroge pia akiongea katika Kaunti ya Meru wakati wa mkutano wao wa kisiasa alisema suala la mgombeaji wao wa urais lishaamuliwa.
“Wafuasi wetu wameweka wazi kuwa wanayemtaka ni Sifuna. Hilo limethibitishwa kupitia mikutano yetu maeneo mbalimbali nchini,” akasema Bi Njoroge.
Bw Orengo pia alisema jamii mbalimbali zina haki ya kufanya mashauriano kuhusu maslahi yao ya kisiasa, akitaja mijadala inayoendelea Mlima Kenya na Ukambani.
Kando na kambi ya Bw Sifuna, azma ya Bw Orengo pia imewachemsha viongozi kutoka Nyanza wanaounga mkono kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto.
Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi amemshutumu Bw Orengo kwa kutumiwa kugawanya kura za Waluo, akilinganisha hali hiyo na uchaguzi wa 2002.
“Jinsi alivyotumiwa na Daniel arap Moi kugawanya kura zetu 2002, sasa anatumika tena na Uhuru kugawanya kura zetu, lakini hilo halitatokea,” akasema Bw Wandayi.
Waziri huyo pia alisema viongozi wa Siaya wamekubaliana kumuunga mkono Rais Ruto na sasa wanamakinikia usajili wa wapiga kura.
Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga, pia amepuuzilia mbali uwezekano wa Bw Orengo kushinda urais, akisema hana umaarufu wowote wa maana nchini.
Huku mjadala ukiendelea, Linda Mwananchi pia inajaribu kujigeuza kutoka jukwaa la kisiasa hadi chama kitakachoshiriki uchaguzi wa 2027.
Hata hivyo, ombi lake la kuhifadhi jina Linda Mwananchi Party lilikataliwa na Afisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, hatua ambayo imeongeza changamoto kwa vuguvugu hilo.
Bw Orengo pia alitetea uamuzi wake wa kukosa mkutano wa Linda Mwananchi Meru mnamo Jumapili akisema haikuhusiana na ubabe kati yake na Bw Sifuna.
“Nilikuwa na shughuli nyingine nzito na Babu aliwasilisha salamu na udhuru wangu. Bado namakinikia wazo la kuwa na mgombeaji mmoja wa upinzani,” akasema.
Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Chris Omore naye anasema ukosefu wa chama thabiti huenda ukalemeza azma ya Mabw Orengo na Sifuna kumpa Rais Ruto upinzani mkali 2027.