Habari za Kitaifa

Wauguzi wavamiwa na wahuni Kisii wakijiandaa kuwasilisha malalamishi kwa serikali

Na WAANDISHI WETU September 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAUGUZI wanaoendelea na mgomo katika Kaunti ya Kisii, jana walishambuliwa na watu wanaodaiwa kuwa wahuni walipokuwa wakijiandaa kushiriki mgomo wa amani na kuwasilisha malalamishi yao kwa serikali ya kaunti hiyo.

Walishambuliwa katika uwanja wa Hospitali ya Rufaa ya Kisii, tukio ambalo viongozi wa muungano wao walilikemea na kulitaja kuwa la kuhofisha mno.

Wauguzi ambao hawakutaka kutajwa, walisema wanaume wapatao 40 waliojihami kwa mipini ya majembe walivamia walipokuwa wakijiandaa kuandamana.

Katibu Mkuu wa Muungano wa Wauguzi (KNUN), Seth Panyako, alitaja shambulizi hilo kuwa la kipuzi, akilalamika kuwa polisi waliofahamishwa awali kuhusu mipango ya maandamano hayo walifeli kuwalinda wauguzi.

“Polisi Kisii wameingiliwa. Tulitoa notisi bayana kwa polisi kuwa tutafanya maandamano ya amani. Maafisa wa polisi walikuja lakini badala ya kutoa ulinzi, waliagiza wauguzi kuondoka, wakisema ikiwa watakaidi, wahuni hao wa kulipwa wataachiliwa kwao,” akasema Bw Panyako akihutubia vyombo vya habari.

“Tunalaani vikali tukio hili. Tunauliza polisi mjini Kisii kwa nini waliruhusu wahuni kushambulia wauguzi wasio na fujo, kana kwamba hawaugui. Hatutakuwa na huruma kwa wasio na huruma nasi. Sisi ni wauguzi; wanaweza kuwa na bunduki na silaha, lakini tunaweza pia kuwa hatari.”

Homabay, wauguzi wameapa kukaidi wito wa Baraza la Magavana (CoG) kurejea kazini huku majadiliano yakiendelea.

Mwenyekiti wa Baraza, Bw Ahmed Abdullahi, aliwahimiza wauguzi nchini kote kurejelea majukumu yao huku magavana wakishughulikia malalamishi yao.

Gavana huyo wa Wajir, alisema baraza limejadili Mkataba wa Makubaliano kuhusu Malipo (CBA) lakini baadhi ya kaunti zimeshindwa kuutekeleza, huku wauguzi wakisema hawatasikiza ombi hilo.

Mkurugenzi wa Muungano Kitaifa wa Wauguzi na Wakunga (KNUNM) tawi la Homa Bay, Emmadick Okeyo, alisema kususia kazi ndiyo hatua yao.

“Hatutarejea kazini hadi malalamishi yetu yatakaposhughulikiwa,” akasema Bw Okeyo.

Mwenyekiti wa tawi hilo, Bw Enock Ocharo aliitaka CoG kukoma kuwatishia wauguzi.

“CoG ijishughulishe na kuangazia malalamishi yetu. Vitisho wanavyotoa havina athari yoyote,” akasema Bw Ocharo.

Kisumu, baadhi ya wagonjwa wanageukia maduka ya kuuza dawa huku mgomo unaoendelea wa wauguzi ukitatiza huduma katika hospitali ya rufaa Kisumu.

Wauguzi wanataka mkataba wao wa CBA utiwe saini ili uthibitishwe kisheria. Mkataba huo unatoa mwongozo kuhusu maendeleo kitaaluma, marupurupu na malipo mengineyo.

Aidha, wanataka wenzao walioajiriwa chini ya mpango wa Afya kwa Wote (UHC) wakati wa hatamu ya Rais mstaafu Uhuru Kenyatta kuajiriwa kwa kandarasi za kudumu.

Wauguzi wa UHC kwa sasa wameajiriwa kwa kandarasi za muda.

Wanaitisha vilevile utekelezaji kamili wa Muafaka wa Kurejea Kazini 2017 uliotiwa saini kati ya muungano wao na CoG.