Habari za Kitaifa

Baraza la Waluo lapoteza ushawishi wazee wakizozania uongozi

Na GEORGE ODIWUOR September 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JAMII ya Waluo inakabiliwa na mgawanyiko mkubwa wa uongozi, wazee wakigawanyika katika makundi mawili yanayodai kumtambua kiongozi halali wa Baraza la Wazee wa Waluo.

Upande mmoja unaongozwa na Nyandiko Ongadi huku mwingine ukiongozwa na Odungi Randa. Wote wanajitambua kuwa Ker halali na walezi wa utamaduni wa jamii hiyo.

Mzozo huo umedumu kwa zaidi ya miaka 10 na sasa umeenea hadi mashinani, ambako baadhi ya wazee wamejiunga na Bw Ongadi huku wengine wakimuunga mkono Bw Randa.

Mgawanyiko huo umeibua wasiwasi kwamba baraza hilo limepoteza ushawishi wake katika masuala ya jamii, hasa siasa na uongozi.

Kiongozi wa Bunge la Wananchi Homa Bay Walter Opiyo, alisema baraza hilo haliwezi tena kutoa mwelekeo wa kisiasa kama ilivyokuwa awali.

Alisema ushawishi wa baraza hilo uliimarishwa zaidi na aliyekuwa kiongozi wa ODM, marehemu Raila Odinga.

“Raila alikuwa mwanasiasa pekee aliyejulikana kwa kuendeleza utamaduni. Kifo chake kilifuta yote hayo na sasa baraza limeachwa bila ushawishi wa kisiasa,” akasema Bw Opiyo.

Mkazi wa Kakuajuok, Zedekiah Ouma, alikosoa baadhi ya wazee kwa kuruhusu wanasiasa kuwashawishi kwa fedha.

“Tofauti na wazee wa jamii nyingine kama Wamaasai, wazee wa Luo wamepoteza mwelekeo,” akasema.

Hata hivyo, mbunge wa Homa Bay Mjini Peter Kaluma alitetea baraza hilo, akisema si taasisi ya kisiasa.

“Baraza halijihusishi na siasa na nadhani katiba yao haiwaruhusu kushiriki siasa. Wale unaowaona pamoja na wanasiasa ni baadhi ya wazee wa ukoo ambao wamealikwa na uwepo wao hauwakilishi baraza,” akasema Bw Kaluma.

Mzozo huo ulizuka baada ya kifo cha Ker Riaga Ogalo mnamo Agosti 2015. Bw Ongadi, aliyekuwa naibu wake, aliteuliwa katika hafla iliyofanyika Ofafa Memorial Hall.

Hata hivyo, Bw Randa alichaguliwa kuwa Ker wakati wa Tamasha la Piny Luo Homa Bay mnamo Julai 2023, na kutawazwa rasmi Disemba 22, 2023.

Uteuzi huo ulipingwa vikali na kundi la Bw Ongadi.

Bw Ongadi, ambaye anatoka Kendu Bay, Karachuonyo, anasisitiza kuwa yeye ndiye Ker halali kwa sababu anamiliki cheti cha usajili wa baraza pamoja na hati za wadhamini.

Bw Ongadi pia amesema anapanga kuwaongoza wazee hadi Got Ramogi kwa ajili ya maombi ya kuunganisha jamii.

Hata hivyo, Bw Randa amesema anaunga mkono mazungumzo ya kuleta amani lakini akasisitiza kuwa yeye ndiye Ker halali.

Alimshutumu Bw Ongadi kwa kushikilia stakabadhi za baraza na kusema hakuwepo wakati yeye alipochaguliwa 2023.