Bei ya maziwa yapanda Nyanza na South Rift kufuatia uhaba mkubwa
BEI ya maziwa imepanda katika baadhi ya maeneo ya Nyanza na Kusini mwa Bonde Ufa, hali inayoathiri familia na wafanyabiashara wa bidhaa mbalimbali hasa vyakula.
Katika Kaunti ya Homa Bay, pakiti ya maziwa ya mililita 500 sasa inauzwa kwa Sh70, kutoka Sh55 hadi Sh60.
Wanaopika na kuuza chai wamelazimika kupunguza kiwango cha maziwa wanachotumia ili kudumisha bei na kulinda faida yao.
Pamela Otieno, anayeendesha kibanda cha chakula Homa Bay, alisema bado anauza kikombe cha chai kwa Sh20 lakini amepunguza maziwa anayoweka kwenye chai.
“Nilikuwa naweka pakiti tano za maziwa katika lita 20 za chai, lakini sasa nimepunguza hadi nne,” akasema.
Kutokana na kuadimika kwa maziwa, baadhi ya wateja wameanza kulalamika kuwa chai imepoteza ladha yake ya awali.
Kisumu, Migori na Kisii pia zimekumbwa na mabadiliko ya bei na uhaba wa maziwa. Kule Kisumu, pakiti ya mililita 500 inauzwa kwa Sh80.