Hichilema aapishwa kwa muhula wa pili mpinzani wake mkuu akifungiwa jela
RAIS wa Zambia Hakainde Hichilema Jumanne aliapishwa rasmi kwa muhula wake wa pili huku mpinzani wake mkuu akiwa gerezani akikabiliwa na mashtaka ya uhaini.
Kuapishwa kwake kumekamilisha mchakato wa uchaguzi wa Agosti 13 ambao waangalizi walisema ulikumbwa na dosari kubwa na ukiukaji wa haki.
Hichilema aliingia madarakani mnamo 2021 akiahidi kurejesha demokrasia baada ya kuishutumu serikali iliyotangulia kwa kuiba uchaguzi na kuwafunga wapinzani.
Hata hivyo, waangalizi wa uchaguzi wa ndani na kimataifa wameripoti dosari kadhaa katika uchaguzi huo, zikiwemo madai ya udanganyifu katika hesabu za kura, kukamatwa kwa wabunge wa upinzani, wanajeshi kuwekwa katika vituo vya kupigia kura na kufungwa kwa mahakama.
Mpinzani wake Brian Mundubile na mgombea mwenza wake Makebi Zulu pia walishtakiwa kwa uhaini mwishoni mwa wiki.
Zambia, inazalisha shaba kwa wingi, imekuwa kitovu cha ushindani kati ya China na Amerika kutokana na utajiri wake wa madini.
Nchi hizo mbili zilimpongeza Hichilema kwa ushindi wake na kutuma wawakilishi kwenye hafla ya kuapishwa kwake.
Zambia imekuwa ikifanya uchaguzi tangu miaka ya 1990 ilipokumbatia mfumo wa vyama vingi, ingawa baadhi yake imekuwa na dosari.
Wachanganuzi wanaonya kuwa uchaguzi huu unaweza kuweka mfano utakaowawezesha viongozi wa baadaye kujilazimisha madarakani badala ya kuimarisha demokrasia.
“Hadhi ya Zambia ya kidemokrasia iko hatarini. Hatujawahi kushuhudia mkanganyiko wa aina hii,” akasema mwanahistoria Euston Chiputa.
Alikuwa akirejelea kusimamishwa kwa kuhesabiwa kura, kuwekwa kwa wanajeshi katika vituo vya kuhesabia kura na kukamatwa kwa viongozi wa upinzani.
Waangalizi wa uchaguzi walisema kulikuwa na dalili za kuongezwa kwa kura katika hesabu ya Hichilema, ingawa walikubaliana kuwa angeshinda hata bila kura hizo zinazodaiwa kuongezwa.
Tume ya Uchaguzi ya Zambia ilisema madai yoyote ya udanganyifu yanapaswa kuwasilishwa mahakamani.
Kinaya ni kwamba mahakama ilifungwa siku ya mwisho ya kuwasilisha kesi ya kupinga matokeo. Baadaye zilisema hakuna malalamishi yaliyowasilishwa.
Serikali pia haijatoa maelezo ya kutosha kuhusu mashtaka dhidi ya Mundubile na viongozi wengine 12 wa upinzani waliotiwa gerezani.
Licha ya machafuko ya kisiasa, wawekezaji bado wanaendelea kuonyesha imani kwa uchumi wa Zambia.
Hichilema aliongoza mchakato wa kupunguza deni na kuimarisha uchumi katika muhula wake wa kwanza, hatua iliyomfanya kuwa chaguo linalopendelewa na wawekezaji wanaotaka mwendelezo wa sera.
Hata hivyo, mtafiti wa Chatham House Christopher Vandome alisema mafanikio ya kiuchumi ya muda mfupi hayawezi kuficha madhara ya muda mrefu ya kuangamiza taasisi za kidemokrasia.