Wazazi waliotengana kugawana gharama ya malezi kwa usawa, mahakama yaagiza
MAHAKAMA imewaamuru wanandoa waliotengana kugawana kwa usawa gharama ya kuwalea watoto wao watatu, na kukataa ombi la mama kutaka baba abebe mzigo wote wa kifedha.
Hakimu Mkuu wa Mahakama ya Bungoma, T.O. Omono, alisema wazazi wote wana wajibu wa kuwatunza watoto wao, hasa pale ambapo kiwango chao cha mapato ni karibu sawa.
Hakimu huyo aliwaamuru DA na mumewe AW kugawana kwa usawa gharama ya chakula, mahitaji mengine na malezi ya watoto hao.
Pia watachangia kwa usawa karo na gharama nyingine za shule katika shule ambazo watoto hao wanasoma hadi mwisho wa mwaka wa masomo.
Watoto hao, EW, SI na AJ, pia watabaki katika makazi yao ya sasa hadi kesi kuu itakaposikizwa na kuamuliwa.
DA alikuwa ameomba mahakama imwamuru AW kutoa pesa kila mwezi za chakula, karo, matibabu na mahitaji mengine ya watoto.
Alidai amekuwa akigharamia mahitaji ya watoto peke yake licha ya mumewe kuwa mfanyakazi wa Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF).
AW alikanusha madai hayo na kusema tayari alikuwa akigharamia mahitaji ya watoto.
Alisema pia alikuwa akigharamia matibabu yao kupitia bima yake ya afya.
Mahakama ilibaini kuwa mahitaji ya matibabu ya watoto hao tayari yalikuwa yakigharamiwa kupitia bima ya baba yao.
Hata hivyo, hakimu alisema hilo halimaanishi kuwa baba anapaswa kuachwa peke yake kugharamia mahitaji mengine.
Mahakama ilichunguza taarifa za kifedha zilizowasilishwa na wazazi hao na kubaini kuwa mapato yao ya kila mwezi yalikuwa karibu sawa.
DA alisema katika hati yake kwamba, alikuwa akipata mshahara wa Sh27,669 kwa mwezi baada ya makato.
Baba pia aliwasilisha taarifa kuhusu mshahara wake wa KDF, matumizi na majukumu mengine ya kifedha.
Hakimu alikataa hoja ya mama kwamba baba anapaswa kuwalea watoto hao peke yake.