Siasa

Visiki vya Kalonzo kuingia Ikulu 2027

Na BENSON MATHEKA September 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KINARA wa Wiper Patriotic Front, Kalonzo Musyoka, ana uzoefu, ngome ya kisiasa ya kuaminika na nafasi nzuri katika kinyang’anyiro cha kutafuta mgombeaji urais wa upinzani mwaka 2027.
Lakini wachambuzi wa siasa wanasema safari yake ya Ikulu sasa inakabiliwa na mtihani mkubwa. Baada ya miaka mingi akiwa katikati ya siasa za kitaifa, Kalonzo atalazimika kuthibitisha kwamba ana uwezo wa kujenga uungwaji mkono nchini kote, wala si kutegemea hadhi yake au uzoefu au huruma ya kisiasa.
Kalonzo alikuwa Makamu wa Rais wakati wa utawala wa marehemu Mwai Kibaki kuanzia 2008 hadi 2013.
Pia alikuwa mgombea mwenza wa Raila Odinga katika uchaguzi wa urais wa 2013 na 2017.
Hata hivyo, mwaka 2022 Raila aliteua Martha Karua kuwa mgombea mwenza wake.
“Historia hiyo imempa Kalonzo uzoefu mkubwa katika kampeni za urais na kujenga miungano ya kisiasa. Lakini 2027 anahitaji kubadilisha historia hiyo ili kuwa kinara wa kivumbi cha urais wa upinzani,” asema mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
Uchunguzi wa shirika la maoni la Infotrak uliochapishwa Julai ulimweka Kalonzo katika nafasi ya kwanza – asilimia 27 – miongoni mwa wanaotajwa kugombea urais kwa tikiti ya muungano wa upinzani.
“Lakini kura hizo pekee haziwezi kumhakikishia tiketi ya upinzani,” asema Gichuki.
Ngome moja tu
Ngome ya Kalonzo imekuwa Machakos, Kitui na Makueni. Kaunti hizo zilikuwa na zaidi ya wapigakura 1.6milioni waliosajiliwa katika uchaguzi wa 2022.
Japo wachambuzi wanasema huo ni msingi mkubwa, wanatahadharisha kwamba mgombea urais hawezi kutegemea eneo moja pekee.
“Kalonzo atalazimika kutanua ushawishi wake hadi Magharibi, Nyanza, Bonde la Ufa, Pwani, Mlima Kenya, Nairobi na Kaskazini Mashariki,” asema mchanganuzi Job Kimanzi.
 Changamoto nyingine ni kizazi kipya cha wapigakura. Takwimu za IEBC zinaonyesha vijana ni sehemu kubwa ya wapigakura waliosajiliwa.
Maandamano ya Gen Z mwaka 2024 yalionyesha wazi kwamba vijana wanaweza kujipanga kitaifa bila kutegemea vyama vya jadi.
Hilo linabadilisha kabisa mchezo wa kisiasa. Kalonzo sasa atalazimika kueleza kwa nini uzoefu wake serikalini unafaa kwa kijana wa miaka 25 anayekabiliwa na ukosefu wa ajira, kodi kubwa na gharama ya maisha.
Ushindani upinzani
Kalonzo pia anakabiliwa na ushindani kutoka kwa vigogo wenza wa upinzani wanaojikuza.
Gachagua amekuwa akifanya mikutano ya kisiasa na mashauriano katika maeneo mbalimbali, huku pia akilenga Wakenya wanaoishi nje ya nchi.
Kwa upande mwingine, kundi la Linda Mwananchi linaloongozwa na Sifuna limechagua mkakati wa kufika mashinani. Kundi hilo limefanya mikutano Magharibi, Nyanza, Pwani na hivi karibuni Meru.
Kalonzo naye ameanzisha jukwaa la kidijitali la Komboa Kenya, akazindua Bajeti ya Mwananchi na kufanya kampeni katika baadhi ya maeneo nje ya Ukambani. Amefanya pia mikutano na viongozi wa Linda Mwananchi.
Hata hivyo, kasi ya shughuli hizo ndiyo itakuwa muhimu. Mgombea urais hawezi kuonekana kutumia muda mwingi kujadili uundaji miungano kuliko kukutana na wapigakura nyanjani.
Vijana na siasa mpya
Maandamano ya 2024 yalionyesha kuwa siasa za Kenya zinaingia katika awamu mpya. Vijana walijipanga kupitia mitandao ya kijamii na majukwaa mengine bila kutegemea miundo ya vyama vya kisiasa.
Maandamano hayo yalifika kaunti nyingi nchini na kuibua masuala ya gharama ya maisha, ukosefu wa ajira, ufisadi na kutengwa kwa vijana katika maamuzi ya nchi. Kwa Kalonzo, hii ina maana kuwa uzoefu wake wa kisiasa pekee hautoshi. Anahitaji sera zinazogusa maisha ya vijana. Ajira, teknolojia, biashara, elimu, uwajibikaji na mageuzi ya taasisi zinapaswa kuwa sehemu ya ujumbe wake.
Zaidi ya hayo, vijana wanataka nafasi ya kushiriki katika siasa, si kuwa watazamaji au wapigakura wakati wa uchaguzi pekee.
Kalonzo anaweza kufaidi kutokana na uzoefu wake, ngome ya kisiasa na nafasi yake katika kura za maoni. Lakini hakuna moja kati ya mambo hayo yanampa tikiti ya urais moja kwa moja.
Anahitaji kuonyesha kwamba anaweza kupata kura nje ya Ukambani. Anahitaji kujenga miundo ya Wiper katika maeneo mapya, kuvutia viongozi wenye ushawishi na kuonyesha kuwa chama kina uwezo wa kupiga kampeni ya kitaifa.
Upinzani nao unahitaji kuchagua mgombea kwa kuangalia uwezo wa kufika maeneo mengi, nguvu za mashinani, uwezo wa kujenga miungano, sera na uwezo wa kuvutia wapigakura ambao bado hawajaamua.
Uzoefu wa Kalonzo akiwa makamu wa rais ni wa kuendesha serikali. Ngome yake ya kisiasa inampa nguvu ya kuketi meza ya kujenga. Kura za maoni zimempa mwanzo mzuri.
Lakini hayo yote hayatoshi. Muda wa kulinda ngome, kufikia wapigakura wasio na msimamo, kushawishi vijana na kupanua Wiper kote nchini ni sasa.
Aliyekuwa Waziri wa Usalama Fred Matiang’i alikuwa na asilimia 26, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna asilimia 19, huku aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua akiwa na asilimia tisa.