Uncategorized

Ruto abadili msimamo kuhusu kampuni ya Tata Chemicals

September 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto amesema kandarasi ya uchimbaji wa madini katika eneo la Magadi itatangazwa upya kupitia zabuni yenye ushindani, hatua inayofungua fursa kwa kampuni nyingi kushiriki katika shughuli hiyo na kukomesha udhibiti wa muda mrefu wa kampuni ya Tata Chemicals ya India.

Akizungumza Jumamosi katika Kaunti ya Kajiado wakati wa kuzindua mradi wa kuweka lami barabara ya Ngong-Kibiko-Kangeria, Rais Ruto alionekana kubadili msimamo wake wa awali aliotoa Loitokitok kwamba tayari kampuni mpya ilikuwa imepatikana kuchukua nafasi ya Tata Chemicals.

Wizara ya Madini ilisimamisha leseni ya kampuni hiyo mwezi Julai kutokana na madai ya kutofuata masharti ya kisheria na kiutendaji.

Rais Ruto alisema kandarasi ya sasa ya Tata Chemicals haiwezi kuendelea, akisisitiza kuwa rasilimali za Magadi zinafaa kushughulikiwa na kampuni kadhaa kwa wakati mmoja.

“Tutatangaza zabuni upya ili kampuni nyingine, si kampuni moja pekee, bali kampuni tatu, nne, tano, sita au hata kumi ziweze kuomba. Rasilimali tuliyo nayo Magadi ni kubwa kutosha kuhudumia zaidi ya kampuni moja,” alisema.

Aliongeza kuwa serikali itahakikisha kuwa shughuli za uongezaji thamani madini hayo zinafanyika nchini Kenya badala ya nje ya nchi.

“Safari hii tutahakikisha uongezaji thamani wa rasilimali za Magadi unafanyika hapa Kenya,” alisema.

Haikufahamika mara moja iwapo Tata Chemicals itaruhusiwa kushiriki katika zabuni hiyo mpya.

Rais pia alitangaza kuwa serikali inapanga kuanzisha kiwanda cha kutengeneza vioo na kemikali ili kuongeza ajira kwa Wakenya.

Aidha, alisema asilimia 70 ya ekari 24,000 ambazo Tata Chemicals imekuwa ikitumia chini ya makubaliano ya ardhi zitarejeshwa kwa jamii ya Kaunti ya Kajiado.

“Hakuna kampuni itakayomiliki ekari 24,000 za ardhi ya Kajiado. Huenda wakatumia asilimia 20 au kiwango cha juu cha asilimia 30 pekee. Angalau asilimia 70 ya ardhi hiyo itarejeshwa kwa wananchi,” alisema.

Rais alikosoa viongozi wa upinzani waliompinga kuhusu hatua dhidi ya Tata Chemicals, akisema wanatetea maslahi ya wafadhili wao badala ya maslahi ya wananchi.

Kauli hiyo ilijiri siku moja baada ya viongozi wa upinzani akiwemo Kalonzo Musyoka na Seneta Edwin Sifuna kumshutumu Rais kwa madai ya kuwatisha wawekezaji kwa maslahi binafsi.

Ruto alisema hatatishwa katika juhudi za kuhakikisha biashara kati ya Kenya na mataifa mengine inakuwa ya usawa.