Habari

Nyoro:Tutamshinda Ruto kura ya 2027 na kuokoa nchi

Na GEORGE MUNENE September 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KIONGOZI wa People’s Party, Ndindi Nyoro amesema yuko tayari kuwania urais mwaka 2027 chini ya muungano wa upinzani, akisema ana uwezo wa kumshinda Rais William Ruto.
Bw Nyoro alisema Jumapili kwamba iwapo muungano huo utamteua kuwa mgombea wake wa urais, atakabiliana na Rais Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.
“Ninafaa kuwa Rais wa Kenya,” alisema Bw Nyoro alipohutubia mikutano ya hadhara katika maeneo ya Kangaita na Mukinduri, Kaunti ya Kirinyaga.
Alisema adui wa pamoja wa vyama vya upinzani ni Rais Ruto na akaahidi kwamba iwapo atateuliwa, atamshinda na kumrudisha nyumbani kwake Sugoi.
“Ikiwa muungano wa upinzani utakubaliana kwamba mimi ndiye mgombea wa kuwania urais dhidi ya Ruto, nitapambana naye na kumshinda,” alisema.
Bw Nyoro alijigamba kuwa ana rekodi ya kuchapa kazi na akasema akipewa nafasi ya kuongoza Kenya, anaweza kubadilisha maisha ya wananchi ndani ya mwaka mmoja.
Alitaja miradi ya elimu katika eneo lake la uchaguzi kama mfano wa uwezo wake wa kuleta mabadiliko.
 “Katika eneo langu nimehakikisha hali katika shule za upili ni nzuri. Wanafunzi hulipa Sh500 pekee kwa muhula na chakula hutolewa bila malipo,” alisema.
 Aliongeza kuwa ameboresha shule za msingi za umma na mazingira kwa wanafunzi.
“Mimi ni mchapa kazi na ninapaswa kupewa nafasi ya kuongoza Kenya kwa manufaa ya Wakenya wote,” alisema.
Bw Nyoro pia alionyesha matumaini kwamba vyama vya upinzani vitaafikiana na kuteua mgombea mmoja wa urais.