Siasa

Wabunge wa Mulembe wamuitisha Ruto kiti cha Kindiki kabla wapige kampeni ya ‘Tutam’

September 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WABUNGE kutoka eneo la Magharibi wamempa Rais William Ruto orodha ya matakwa wanayotaka yashughulikiwe kabla ya eneo hilo kumuunga mkono katika uchaguzi wa 2027.

Miongoni mwa matakwa makuu ni wadhifa wa Naibu Rais ambao wanataka utengewe mwanasiasa kutoka Magharibi katika muhula wa pili wa Rais Ruto.

Pia wanataka eneo hilo kuhifadhi nafasi yake katika Tume ya Huduma za Bunge na miradi ya Serikali iliyokwama ikamilishwe.

Wabunge hao pia wanataka Serikali kuingilia kati matatizo yanayokumba sekta ya sukari, kushughulikia mzozo wa ufadhili wa elimu na kuweka umeme katika maeneo ambayo bado hayajaunganishwa.

Matakwa hayo yaliafikiwa Jumatatu wakati wa mkutano wa wabunge wa Magharibi uliofanyika Kisumu ulioandaliwa na Waziri wa Vyama vya Ushirika, Bw Wycliffe Oparanya.

Kuhusu wadhifa wa Naibu Rais, wabunge hao walisema: “Kama jamii ya Magharibi, tunataka wadhifa wa Naibu Rais ili kumsaidia Rais William Samoei Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.”

Mwenyekiti wa Kundi la Wabunge wa ukanda wa Magharibi, Bw John Waluke, alisema wanataka wadhifa huo kwa niaba ya eneo hilo bila kumuunga mkono mwanasiasa yeyote kwa sasa.

Msimamo huo ni tofauti na ule wa Mei ambapo wabunge hao walimuunga mkono Bw Oparanya kwa kiti hicho.

Wabunge hao pia walitaka nafasi inayoshikiliwa na Bi Rachael Ameso katika Tume ya Huduma za Bunge ibaki mikononi mwa mwakilishi kutoka Magharibi.

Walitaka pia miradi ya Serikali iliyokwama ikamilishwe katika eneo hilo na Serikali itafute suluhu ya changamoto zinazowakabili wakulima na viwanda vya sukari.

Hata hivyo, walipinga vikali Mswada wa Marekebisho ya Mazao.

“Serikali inapaswa kushughulikia masuala yanayoathiri sekta ya sukari. Hata hivyo, tunasisitiza kuwa tunapinga kabisa Mswada wa Marekebisho ya Mazao,” walisema.

Wabunge hao pia walitaka Serikali ishughulikie tatizo la ufadhili wa elimu, wakisema wanafunzi kutoka familia maskini ndio wanaoathirika zaidi.

Walipendekeza usajili wa wapigakura uendelezwe kwa pamoja na kampeni za kuwahamasisha wananchi ziongozwe na wabunge.

Aidha, walitaka Wizara ya Kawi kuunganisha umeme katika maeneo ambayo bado hayana huduma hiyo na kutatua hitilafu za mara kwa mara.

Bw Oparanya alisema viongozi hao wataendelea kufanya mikutano ili kuimarisha uungwaji mkono wa Rais Ruto.

“Tutakuwa na mikutano ya mara kwa mara kujitayarisha kwa uchaguzi mkuu ujao. Viongozi wote mnaowaona hapa wanampigia debe Rais Ruto kwa muhula wa pili,” alisema.

Wabunge 22 walihudhuria mkutano huo, huku watano wakisema hawangefika kwa kuwa walikuwa nje ya nchi.

Mbunge wa Budalang’i, Bw Raphael Wanjala, alisema Magharibi ina haki ya kudai kiti cha Naibu Rais kwa kuwa liliunga ODM na marehemu Raila Odinga kwa muda mrefu.

Alisema viongozi wa eneo hilo wamekubaliana kudai kiti hicho katika muungano wowote utakaohusisha ODM.