Habari za Kaunti

Shahbal amkaidi Ruto, atema ODM na kuapa kuwania ugavana Mombasa

Na WINNIE ATIENO September 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UAMUZI wa mfanyabiashara na mwanasiasa Suleiman Shahbal kukataa jaribio la Rais William Ruto kumshawishi asigombee ugavana wa Mombasa, na kutangaza kujiondoa katika Chama cha ODM, kumesababisha mwelekeo mpya wa kisiasa katika ushindani wa ugavana wa kaunti hiyo.

Awali, Bw Shahbal alitarajiwa kushindania tikiti ya ODM dhidi ya Gavana Abdulswamad Nassir kuwania ugavana 2027, kabla Dkt Ruto kujaribu kumshawishi ajiondoe kwenye kinyang’anyiro Jumanne.

Katika mahojiano na wanahabari wa Mombasa Jumatano usiku, mwanasiasa huyo alisisitiza atakuwa debeni hata kama ODM haitampa tikiti.

Alidai kuwa, Rais Ruto alishawishiwa na watu wanaotaka kumtoa kwenye kinyang’anyiro hicho.

“Ninaamini Rais alichochewa kutamka maneno hayo, kwamba mimi ni mfanyabiashara na ninapaswa kuwaachia wanasiasa siasa. Ndiyo maana wanasukuma suala la kugawana maeneo. Kwa nini hamwaachi wananchi waamue?” Bw Shahbal alisema.

Huku akitangaza kujiondoa kutoka ODM, alisema anaamini chama hicho hakitamteua.

“Tuko katika ‘talaka ya kirafiki’ na ODM. Chama hakitaniteua na ninajiandaa na jukwaa jipya la kisiasa. Tuna chama chetu cha kisiasa ambacho tutakitangaza hivi karibuni,” Mjumbe huyo wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) alisema.

Katika uchaguzi wa mwaka wa 2022, Bw Shahbal alijiondoa katika kinyang’anyiro cha ugavana na kumuunga mkono Bw Nassir.

Jumanne, Rais Ruto alimshauri kutorejea katika kinyang’anyiro hicho, akisema Kenya ingenufaika zaidi kutokana na ujuzi wake wa biashara, uwekezaji na uundaji wa nafasi za ajira kuliko kuingia katika siasa.

Rais alikuwa akizungumza wakati wa kutiwa sahihi kwa makubaliano ya Sh12 bilioni kati ya GulfCap Group ya Bw Shahbal na kampuni ya kimataifa ya shughuli za bandarini ya DP World, kwa ajili ya kuanzisha eneo maalumu la kiuchumi lenye ukubwa wa ekari 535 Jomvu.

Bw Shahbal alikiri kuwa ana urafiki na Dkt Ruto na akamsifu Rais kwa kutambua mafanikio yake katika biashara. Hata hivyo, alisema hakubaliani na ushauri wa kuachana na siasa.

Alihoji kwa nini Rais, ambaye pia ni mfanyabiashara, angemwomba achague kati ya biashara na uongozi wa kisiasa.

Kulingana naye, wanasiasa wengi wa Kenya wamewekeza katika biashara, akisema biashara na siasa zina malengo tofauti.

“Unajua biashara ni jambo la kibinafsi; unapata hasara na faida ambazo hunufaisha familia yako na wafanyakazi wako. Lakini katika siasa, unapogombea uongozi, ni tendo la kujitolea kuwahudumia wananchi,” alisema.

Alikosoa ODM kwa kutumia vibaya uteuzi wa wagombea kwa manufaa ya watu wachache, akidai kwamba baadhi ya madiwani waliotaka kumuunga mkono mwaka wa 2022 walitishiwa kunyimwa tiketi za chama.

“Enzi ya kuamua wanasiasa wanaopaswa kugombea na wale wanaopaswa kujiondoa imepitwa na wakati,” alisema.

Uamuzi wake wa kuondoka katika chama hicho unaweza kujaribu uwezo wake wa kujenga nguvu za kisiasa nje ya chama ambacho kimekuwa nguvu kubwa katika siasa za Mombasa kwa zaidi ya muongo mmoja.

Hata hivyo, Bw Shahbal amekuwa akitumia vyama tofauti katika azma zake za uongozi, vikiwemo Wiper na Jubilee, tangu mwaka 2013.

Alikanusha pia uwezekano wa kukubali nafasi ya uwaziri iwapo atapewa.

Bw Shahbal anasema hagombei wadhifa huo kwa ajili ya kujipatia fedha, bali anataka kuwatumikia wananchi.

Amependekeza kutengwa kwa Sh50 milioni kila mwaka kwa kila wadi kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika sekta za afya, vijana, wanawake na usalama, akisema rasilimali zinapaswa kugawanywa moja kwa moja zaidi hadi ngazi ya mashinani.