Maeneo hatari El- Nino ikitarajiwa hivi karibuni
KENYA inakabiliwa na hatari aina tatu za mafuriko wakati wa msimu wa mvua miezi ya Oktoba, Novemba na Desemba, huku hali ya El Niño ikiimarika na baadhi ya maeneo tayari yakianza kupokea mvua kubwa.
Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) limesema kuna uwezekano wa karibu asilimia 100 kwamba, hali hiyo itaendelea hadi Februari 2027.
Nchini Kenya, El Niño inahusishwa na mvua nyingi kuliko kawaida katika maeneo mengi.
Takriban watu milioni 1.5 katika kaunti zote 47 wanaweza kuathirika, kwa mujibu wa tathmini ya awali ya serikali. Hata hivyo, ripoti kamili kuhusu maandalizi ya nchi bado haijakamilika.
Mamlaka ya Hali ya Hewa Kenya (KMSA) imetambua hatari ya mafuriko mijini, mafuriko ya mito na mafuriko ya ghafla. Hatari hizi zinatofautiana kulingana na aina ya ardhi, mifumo ya mitaro na ukaribu wa mito na maziwa.
Zacharia Mwai, mkurugenzi msaidizi wa Huduma za Hali ya Hewa na Maji katika KMSA, alisema Nairobi ni miongoni mwa maeneo yaliyo katika hatari kubwa ya mafuriko mijini.
Mito ya Nairobi, Mathare na Mbagathi ni miongoni mwa maeneo yanayofuatiliwa. Ramani iliyofanywa na Kituo cha Kitaifa cha Operesheni za Maafa, Shirika la Msalaba Mwekundu na Idara ya Usimamizi wa Maafa ya Kaunti ya Nairobi imetambua maeneo 246 yanayoweza kuwa hatarini.
Katika maeneo ya mijini, majengo na barabara nyingi zenye lami huzuia maji kupenya ardhini. Hivyo, mvua kubwa huongeza kiwango cha maji yanayotiririka na kuzidisha shinikizo kwenye mabomba.
Eneo la Nyali, Mombasa, ambalo limekuwa likikumbwa na mafuriko mara kwa mara, pia limetajwa kuwa eneo hatari. Kisumu ni miongoni mwa miji inayofuatiliwa kutokana na uwezekano wa mafuriko.
Lakini hatari hiyo haiko mijini pekee. Bonde la Tana ni miongoni mwa maeneo yanayotarajiwa kuathirika zaidi. Eneo la chini la Tana linaanzia karibu na Garissa na kuendelea hadi Madogo, Bura, Hola na delta ya Tana.
Delta ya Tana ni eneo hatari kwa sababu ardhi yake ni tambarare. Wakati wa mvua za El Niño za 2023/2024, baadhi ya maeneo yalikatizwa na mafuriko.
Katika Magharibi mwa Kenya, Bonde la Mto Nzoia, hasa maeneo ya Budalangi na Bunyala, pia liko hatarini. Maji kutoka Ziwa Victoria yanaweza kurudi kwenye mto na kuongeza hatari kwa wakazi wanaoishi karibu na mto.
Mito ya Nyando na Yala pia imetajwa miongoni mwa maeneo yanayoweza kukumbwa na mafuriko.
Katika Bonde la Ufa, Narok ni miongoni mwa maeneo yaliyotajwa kuwa hatarini. Mito mingine kama Ewaso Ng’iro inaweza pia kusababisha mafuriko ya ghafla, hasa karibu na Isiolo, ambapo maji yanaelekea Lorian Swamp.
Kaskazini mwa Kenya, Turkana, Wajir, Mandera, Marsabit na Garissa zinakabiliwa na hatari ya mafuriko ya ghafla kutokana na kuwepo kwa mito ya msimu.
Maeneo haya yanaweza kupokea mvua nyingi baada ya kipindi kirefu cha ukavu. Maji yanaweza kutiririka kwa kasi kabla hayajapenya ardhini, na kusababisha mafuriko ya ghafla.
Kitui na maeneo mengine ya mashariki mwa Kenya pia yana mito mikubwa ambayo huwa mikavu kwa muda mrefu lakini hujaa maji kwa kasi mvua inaponyesha.
Serikali imeanza maandalizi ya kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na mvua hiyo. Lengo ni kuepuka madhara yaliyotokea wakati wa mvua ya 2023/2024 ambayo ilisababisha hasara kubwa.