Madai ya Omar kuhusu wafu kushiriki kura kumpa Ruto Tutam yazua gumzo
UCHAGUZI Mkuu wa 2027 umeingia katika mdahalo mpya baada ya Katibu Mkuu wa UDA, Hassan Omar, kudai kwamba hata wapiga kura waliokufa wanaweza kutumiwa katika juhudi za kumhakikishia Rais William Ruto ushindi.
Kauli hiyo aliyotoa Mombasa Ijumaa imezua mjadala mkali kuhusu uaminifu wa uchaguzi wa 2027, huku masuala ya sajili ya wapiga kura, taarifa za vitambulisho vya waliofariki na matumizi ya teknolojia ya kibayometriki yakipewa uzito mpya.
Bw Omar alionekana kudokeza kuwa mianya katika mfumo wa uchaguzi inaweza kutumiwa kwa kutumia utambulisho au taarifa za kibayometriki za watu waliokufa ili kuongeza kura katika uchaguzi wa urais na nyadhifa nyingine.
“Siku ya uchaguzi, hata sisi lazima tupambanie kila kura. Hata kama mtu amefariki, tuchukue kidole chake kabla hajazikwa, tukitumie katika mfumo wa BVR na tupige kura hata kama mtu huyo amefariki siku hiyo hiyo,” alisema Bw Omar.
Kauli hiyo inatarajiwa kuzua mjadala mkali huku vyama vya kisiasa vikijipanga kwa uchaguzi ambao tayari umeanza kuonekana kuwa wenye ushindani mkubwa.
Bw Omar aliunganisha madai hayo na azma ya kuhakikisha Rais Ruto anahifadhi kiti chake na washirika wake wanapata nafasi kubwa zaidi katika serikali ijayo.
“Hata yule tunayemzika leo, hiyo kura ndiyo risasi yetu, ngao yetu. Haiwezekani kurudi tena pale tulipokuwa,” akaongeza.
Alisema kuwa kuongeza idadi ya watu waliosajiliwa kuwa wapiga kura kungeipa serikali nafasi kubwa ya kudai nyadhifa zaidi, zikiwemo nafasi za uwaziri na nyadhifa nyingine za juu serikalini.
Kauli hizo zimeibua maswali iwapo Bw Omar alikuwa akionya kuhusu mianya inayoweza kutumiwa katika uchaguzi au alikuwa akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha kila kura inahesabiwa katika kampeni za 2027.
Aidha, zimeibua tena suala la usahihi wa sajili ya wapiga kura, hasa kuhusu kuondolewa kwa majina ya watu waliofariki na usalama wa taarifa zao za kibinafsi.
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) huenda ikakabiliwa na shinikizo zaidi kueleza namna inavyotambua wapiga kura waliofariki na kuwaondoa kwenye sajili, pamoja na hatua zinazochukuliwa kuzuia mtu mwingine kutumia utambulisho wa marehemu kupiga kura.
Suala hilo ni nyeti kutokana na historia ya uchaguzi nchini ambapo madai ya wapiga kura hewa, sajili yenye dosari na udanganyifu wa kura yamekuwa yakizua mivutano mikubwa ya kisiasa.
Kauli ya Bw Omar pia imepewa uzito kwa sababu yeye si mwanasiasa wa upinzani anayekosoa mfumo wa uchaguzi, bali ni Katibu Mkuu wa chama tawala cha UDA.
Wakati huohuo, Bw Omar anajiandaa kuwania tena kiti cha ugavana wa Mombasa, katika kinyang’anyiro kinachotarajiwa kuwahusisha wanasiasa kadhaa wenye ushawishi.
Amekataa wazo la kugawana maeneo ya kisiasa kwa vyama, akisisitiza kuwa wananchi ndio wanaopaswa kuamua viongozi wao.
“Siku ile nilisema hakuna ‘zoning’, akasema atakwenda kuzungumza na boss wangu, sijui ni nani. Hawa ndio boss wangu. Kujeni zungumza na watu hapa,” alisema.