Shahbal aanza kurindima ngoma akilenga ugavana Mombasa
MFANYABIASHARA Suleiman Shahbal ameanza kufufua mtandao wake wa kisiasa katika kaunti ya Mombasa akijitayarisha kwa kinyanganyiro cha uchaguzi mkuu wa 2027, huku akimuonya Rais William Ruto dhidi ya kuteua mgombea mmoja wa ugavana katika eneo hilo.
Bw Shahbal alisema hatua hiyo inaweza kumnyima kura katika kaunti hiyo akimsihi ajifunze kutoka kwa makosa ya marehemu Raila Odinga kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.
Bw Shahbal alimuonya Rais Ruto dhidi ya mipango ya kisiasa inayoweza kuwaondoa wagombea wengine katika kinyang’anyiro cha ugavana ili kumuunga mkono mgombea mmoja anayependekezwa na ikulu.
Alisema kuwa kuwepo kwa wagombea wengi kutamnufaisha Rais kwa kuwa kila mmoja atakuwa akifanya kampeni na kuwahamasisha wapiga kura.
“Ikiwa kuna watu wengi katika kinyang’anyiro, Rais atapata kura nyingi kwa sababu wote watafanya kampeni kwa ajili yake. Lakini ikiwa ni mtu mmoja, ambaye ni mgombea wa Rais hapa Mombasa, wanampotosha Rais,” alisema.
Bw Shahbal, ambaye hivi majuzi alipuuza ushauri wa Rais Ruto wa kutogombea kiti cha ugavana wa Mombasa, alikutana na zaidi ya wanachama 300 wa kundi lake la “Shahbal Movement” katika mkutano ulioandaliwa chini ya kaulimbiu ya “Mombasa is calling” kujadili namna ya kufufua mtandao wake wa kisiasa mashinani.
Alisema mkutano huo haukuwa uzinduzi rasmi wa kampeni yake, bali ulikuwa mwanzo wa maandalizi ya kuimarisha mtandao wake kabla ya kuanza kuwafikia wananchi mashinani.
“Huu ni mkutano wa viongozi wetu wa ‘Shahbal Movement’. Bado sijafanya mkutano wa mashinani. Tutakapoenda kwa wananchi, mambo yatakuwa tofauti kabisa. Nimewaambia watu wangu kwamba kwa miezi mitatu ijayo tunajitayarisha. Hatuna haraka. Tsunami itaanza Januari mwakani,” alisema.
Mfanyabiashara huyo aliwashutumu baadhi ya wanasiasa wanaounga mkono mfumo wa kugawana maeneo ya kisiasa, akisema wanataka kupewa njia rahisi ya ushindi badala ya kwenda mashinani kuwashawishi wapiga kura.
“Upuuzi huu wa kugawana maeneo umeanzishwa na watu wanaoogopa kwenda mashinani kukutana na wananchi. Wanataka usalama; wanataka kupewa njia rahisi ya ushindi,” alisema.
“Ikiwa una imani na uongozi wako, nenda kwa wananchi uwaambie ulichowafanyia nao watakuchagua. Kwa nini una hofu kubwa kiasi cha kutaka kuwazuia watu wengine kugombea?”
Bw Shahbal pia aliwakosoa viongozi wa UDA wanaodai kuwa wanaweza kumhakikishia Rais idadi kubwa ya kura bila kuwepo kwa ushindani.
“Nina hakika watu wa UDA wananisikiliza. Wanampotosha Rais. Hakuna yeyote kati yao anayeweza kuhakikisha kwamba wapiga kura watatoka bila ushindani,” alisema.
Alitaja Nyanza kama mfano, akidai kuwa baadhi ya wagombea wanaopata tiketi ya ODM bila ushindani wa ndani hupoteza ari ya kufanya kampeni.
“Hili ndilo kosa tulilofanya Nyanza. Mara tu mtu anapopewa cheti cha ODM, anapoteza hamu, anarudi nyumbani na kulala kwa sababu tayari ameshinda. Hivyo ndivyo Bw Odinga alipoteza kura Nyanza,” alisema.
Bw Shahbal pia alidai kuwa tiketi ya ODM imekuwa ikitumika Mombasa kuwashinikiza wagombea kuunga mkono chama hicho au kukosa tiketi.
“Safari hii wanaweza kubaki na cheti chao. Sisi tuna mipango,” alisema.
Kauli zake zinajiri wakati ambapo wanasiasa kadhaa wameanza kujipanga kwa uchaguzi wa ugavana wa Mombasa wa 2027.
Miongoni mwa wanaotajwa katika kinyang’anyiro hicho ni Katibu Mkuu wa UDA Hassan Omar, Gavana wa sasa Abdulswamad Nassir wa ODM, Mbunge wa Nyali Mohammed Ali na aliyekuwa Mbunge wa Kisauni Ali Mbogo.
Wiki iliyopita, Bw Omar aliunga mkono uamuzi wa Bw Shahbal kugombea, huku akipinga mikataba ya kisiasa au mfumo wa kugawana maeneo ambao unaweza kuwalazimisha baadhi ya wagombea kujiondoa.