Francis Atwoli: Miaka 25 akipambania wafanyakazi; muhula wa sasa utaenda hadi 2031
ALIANZA kama kijana wa miaka 18 aliyekuwa na kazi katika shirika la posta na mawasiliano.
Hakujua kwamba hatua yake ya kwanza ya kuwakilisha wafanyakazi wenzake ingebadilisha maisha yake na kumweka katika uongozi kwa zaidi ya nusu karne.
Leo, jina la Francis Atwoli ni kubwa katika ulimwengu wa wafanyakazi Kenya.
Kwa miaka 25 amekuwa akiongoza Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi (Cotu-K), akihudumu katika awamu za kisiasa za marais tofauti na misukosuko ya kiuchumi iliyobadilisha maisha ya mamilioni ya Wakenya.
Na Machi mwaka huu, wafanyakazi walimwambia bado hawataki aondoke.
Atwoli alichaguliwa bila mpinzani kwa muhula wa sita wa miaka mitano katika mkutano wa wajumbe wa Cotu uliofanyika Tom Mboya Labour College, Kisumu.
Muhula huo utaendelea hadi 2031.
Kwa mwanamume ambaye amekuwa katika uongozi wa shirika hilo tangu 2001, uchaguzi huo ulikuwa zaidi ya ushindi mwingine.
Ulikuwa thibitisho la uimara wa uongozi wake ndani ya shughuli za wafanyakazi.
Lakini nyuma ya jina la Atwoli kuna safari ndefu. Safari yake katika vyama vya wafanyakazi ilianza baada ya kumaliza shule ya sekondari.
Aliajiriwa na East African Posts and Telecommunication Administration akiwa na umri wa miaka 18.
Ndani ya miezi miwili tu, alichaguliwa bila mpinzani kuwa mwakilishi wa wafanyakazi katika tawi la Nairobi la Union of Posts and Telecommunication Employees.
Akiwa na miaka 21, alichaguliwa kuwa katibu wa tawi la Nairobi. Hapo ndipo safari yake ya muda mrefu katika harakati za wafanyakazi ilipoanza kwa nguvu.
Mwaka 1967, alijiunga rasmi na harakati za wafanyakazi, safari ambayo Cotu baadaye iliitaja alipoadhimisha miaka 50 katika harakati hizo mwaka 2017.
Kwa Atwoli, uongozi haukuwa suala la cheo pekee.Ulikuwa kuhusu uwezo wa wafanyakazi kujitetea.
Alitumwa Italia kusomea masuala ya ajira katika Turin College of Labour Studies, ambako alipata nafasi ya kupanua uelewa wake kuhusu harakati za wafanyakazi duniani.
Aliporudi Kenya, aliendelea na shughuli za chama.Mwishowe, msimamo wake ulimgharimu kazi.
Kwa mujibu wa wasifu wa Cotu, alistaafishwa mwaka 1986 kwa kile kilichoelezwa kuwa kushiriki katika shughuli za chama cha wafanyakazi.
Lakini kuondoka kazini hakukumaliza safari yake.Kulikuwa mwanzo wa hatua nyingine.
Atwoli baadaye akawa Katibu Mkuu wa Kenya Plantation and Agricultural Workers Union (KPAWU).
Alijenga jina katika sekta ya kilimo, hasa katika masuala yaliyohusu wafanyakazi wa mashambani.
Kufikia 2001, alikuwa tayari amejijengea ushawishi mkubwa katika harakati za wafanyakazi.
Mwaka huo, mpenzi huyo wa rhumba alichaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Cotu baada ya kuungwa mkono na vyama 26 kati ya 29 vilivyokuwa wanachama wa shirika hilo.
Huo ulikuwa mwanzo wa enzi yake. Na miaka 25 baadaye, bado yuko katika kiti hicho.
Ingawa Cotu ni shirika la wafanyakazi, Atwoli hakuwahi kujitenga kabisa na siasa za Kenya.
Shirikisho hilo lilifanya kazi pamoja na upinzani wa National Rainbow Coalition (Narc) mwaka wa 2002, uliokuwa ukimuunga mkono Mwai Kibaki katika uchaguzi wa urais.
Kibaki alishinda uchaguzi huo na kumaliza utawala wa Kanu uliokuwa umechukua miaka 40.
Tangu wakati huo, Atwoli amekuwa mtu ambaye kauli zake kuhusu siasa za Kenya zimekuwa zikifuatiliwa kwa karibu.
Huwa anaunga mkono au kukosoa serikali kulingana na masuala yaliyo mbele yake huku akisisitiza lazima Cotu ifanye kazi na serikali iliyo mamlakani kwa maslahi ya wafanyakazi.
Lakini pia amesisitiza kwamba Cotu ni shirika la wafanyakazi na si chama cha kisiasa.
Kwa mujibu wa msimamo rasmi wa Cotu, wanachama wake wana uhuru wa kuunga mkono vyama tofauti, huku shirika likishirikiana na serikali iliyoko madarakani kwa masuala yanayohusu wafanyakazi.
Hapo ndipo moja ya mambo yanayomfanya Atwoli kuwa mtu wa kipekee yanapoonekana.
Anaweza kuwa mkosoaji wa serikali katika suala moja na kuiunga katika suala jingine mradi tu linahusu maslahi ya wafanyakazi.
Kwa miaka yake yote Cotu, suala la mishahara limekuwa mojawapo ya ajenda zake kuu.
Atwoli amekuwa akisisitiza umuhimu wa mshahara wa chini unaomwezesha mfanyakazi kuishi kwa heshima.