Kimataifa

Trump apinga madai China ilisaidia Iran kivita akisisitiza ana ‘uhusiano mzuri’ na Rais Xi

Na REUTERS September 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WASHINGTON, Amerika:

RAIS wa Amerika, Donald Trump mnamo Jumapili alipuuza ripoti kwamba Iran ilipata picha za satelaiti za kambi ya kijeshi nchini Jordan kutoka kwa mashirika ya China kabla ya shambulizi la Julai lililoua wanajeshi watatu wa Amerika.

Ripoti ya jarida maarufu la Wall Street, likiwanukuu maafisa wa Amerika ambao hawakutajwa majina, ilisema picha hizo zilitolewa kwa Iran kabla ya shambulizi hilo kutekelezwa.

Ripoti hiyo haikueleza mashirika ya China yaliyohusika wala kudai kuwa Beijing ilihusika moja kwa moja.

Trump alipoulizwa iwapo angezungumzia suala hilo katika mkutano ujao na Rais wa China Xi Jinping, hakujibu moja kwa moja, bali alitumia ujanja kulinganisha shughuli za ujasusi za China na Amerika.

“Kimsingi wao wanafanya kile tunachofanya. Wanaposema China inatupeleleza, nasema wako sahihi, na sisi pia tunawapeleleza.”

Trump aliwaambia waandishi wa habari akiwa ndani ya ndege ya Air Force One.

Trump pia alisisitiza kuwa ana uhusiano mzuri na Rais Xi, licha ya mvutano wa muda mrefu kati ya Washington na Beijing ambao unaoenekana kuwa ubabe wa kijeshi na kiuchumi.

“Nadhani amekuwa akifanya kila kitu kwa njia inayokubalika, nasi tunafanya kwa njia inayokubalika,” akasema Trump alipokuwa akirejea Amerika baada ya ziara Ireland.

Trump na Xi wanatarajiwa kukutana Amerika mnamo Septemba 24, ingawa China bado haijathibitisha rasmi mkutano huo.

China mnamo Jumatatu ilisema imekuwa ikitimiza wajibu wake wa kimataifa kikamilifu na tena kwa udhabiti ikionekana kujibu madai kuwa inasaidia Iran kwenye vita dhidi ya Amerika.

Msemaji wa Wizara ya Masuala ya Nje Guo Jiakun alisema Beijing inapinga na itaendelea kupinga madai yoyote yasiyo na msingi dhidi yake.

“Tunapinga vikali tuhuma na madai yasiyo na msingi yanayotolewa bila ushahidi,” Guo alisema katika mkutano na waandishi wa habari.

Kauli za Trump zinaonekana kuoana na juhudi za hivi karibuni za utawala wake kupunguza mvutano kati ya Washington na Beijing.

Hii ni licha ya kwamba Amerika haijaridhishwa na uhusiano wa karibu kati ya China na Iran.

Zaidi ya wanajeshi 18 wa Amerika wameuawa tangu vita kati ya Amerika-Israel dhidi ya Iran vilipoanza mnamo Februari 28.