Habari

Hofu genge la ‘panga boys’ likirejea mitaa ya Mombasa

Na WINNIE ATIENO na KARIM RAJAN September 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KWA Said Faiz Khamis, 29, safari ya kawaida ya bodaboda usiku iligeuka kuwa jinamizi baada ya kushambuliwa kwa mapanga na kujeruhiwa kwenye kichwa na vidole.

Mkazi huyo wa Maweni alisema mnamo Septemba 15, saa tano usiku, abiria mmoja alimuomba ampeleke nyumbani kwake eneo la Barsheba, Kisauni.

Bw Khamis alimweleza abiria huyo kuwa angemfikisha steji na hangeingia kwenye kitongoji. Hata hivyo alipomfikisha kwenye steji, abiria alimuomba amfikishe nyumbani kwake, mita chache kutoka steji.

Hata hivyo, alipomfikisha genge la majambazi waliokuwa na silaha walijitokeza na kumvamia.

“Niligundua kuwa abiria alikuwa amepanga watu waliokuwa wanasubiri kunishambulia kwa mapanga. Niliponea chupu chupu na kutoroka lakini nilikuwa nimekatwa katwa kichwani na kwenye vidole. Nilihepa na funguo za pikipiki yangu kwa kutumia vichochoro,” alisema.

Kupitia msaada wa waendesha bodaboda wenzake, alipata pikipiki hiyo katika kituo cha polisi cha Kiembeni mnamo Septemba 17.

Hata hivyo, hii haikuwa mara yake ya kwanza kushambuliwa. Mapema mwaka huu, mwendo wa saa tisa usiku, Bw Khamis alisema alikuwa akimpeleka abiria katika Soko la Kongowea alipovamiwa na vijana waliokuwa kwenye pikipiki.

“Walinipiga kichwani na kunikata kata na kuninyang’anya pikipiki yangu, simu na kila kitu nilichokuwa nacho kilienda. Walimuibia abiria wangu pesa zote ambazo alikuwa anaenda nazo Kongowea kununua bidhaa za biashara,” alisema.

Baada ya kutafuta fedha na kununua pikipiki nyingine, alirejea kazini. Hata hivyo, baada ya kujeruhiwa kwa mara ya pili amemua kuacha kazi hiyo.

“Sasa nimeamua kuacha hii kazi. Kichwa changu kimekatwa vibaya mara mbili. Hii kazi ni hatari sana na nina bahati niko hai,” alisema.

Visa hivyo vimeibua hofu mpya kuhusu mashambulizi ya usiku katika maeneo ya Kisauni huku wakazi na wahudumu wa bodaboda wakidai magenge ya vijana wenye silaha butu yanaendelea kuwahangaisha wakazi.

Mwenyekiti wa kamati ya usalama ya jamii ya Maweni na dereva wa bodaboda, Bw Samson Omondi, alidai kuwa magenge hayo wakati mwingine hutumia wanawake kama chambo.

“Wanawake huwafuata waendesha bodaboda kwenye steji wakitaka huduma zetu. Wanapofikishwa waendako, abiria huchelewesha malipo kwa M-Pesa au kupiga simu, kumbe ni njama ya kuwapa muda washirika wao kujitokeza kutushambulia,” alisema.

Bw Omondi aliwataka maafisa wa polisi kuimarisha operesheni na kuwakamata wanaohusika, akisema baadhi yao wanajulikana na jamii.

Vikundi vya kutetea haki za binadamu pia vimeitaka serikali kuchukua hatua ya kuimarisha usalama.

Mratibu wa Vocal Africa Pwani, Wild Sketty, alisema shirika hilo limeorodhesha watu wanane waliodaiwa kushambuliwa kwa mapanga kati ya saa nne usiku na saa kumi na mbili asubuhi ndani ya wiki moja Kisauni.

Hata hivyo, Naibu Kamishna wa Kaunti ya Kisauni, Bw Jamleck Mbuba, aliwatuliza wakazi akisema polisi tayari wamewakamata baadhi ya washukiwa na wanaendelea kuwasaka wengine.

“Tutawakamata wanaojificha. Tupeni muda, lakini mtusaidie kwa kutoa taarifa ili tuwatambue wahalifu walioko miongoni mwenu,” alisema.